Askofu wa ACK awakosoa Wakenya kwa kumbatiza rais Ruto kwa jina "Zakayo"

“Nakumbuka wakati wa uchaguzi, tulifurahia sana, na unajua serikali ikiingia ni ifanye kazi. Na serikali haina pesa inatoa pesa wapi? Kwetu!” askofu huyo alisema.

Muhtasari

• Askofu alikwenda kwa ndani Zaidi na kunukuu Biblia akisema kwamba Mungu anatoa onyo kali kwa mtu yeyote ambaye anamkosea kiongozi wake heshima.

Askofu Joe Waweru na rais William Ruto
Askofu Joe Waweru na rais William Ruto
Image: Screengrab, Facebook

Askofu wa kanisa la Kianglikana jimbo la Nairobi, Joe Waweru amewakosoa wananchi ambao wanambatiza rais William Ruto kwa jina la ‘Zakayo’ kutokana na uongozi wake kukaza Kamba katika ukusanyaji wa ushuru nchini.

Akizungumza katika hafla ya ibada ya Jumapili ya matende inayoadhimishwa na Wakristo kuelekea Ijumaa ya Pasaka, askofu Waweru alisema kwamba hiyo ni kama kumkosea kiongozi wa nchi heshima.

Askofu Waweru alizungumza katika ibada hiyo iliyohudhuriwa na viongozi wengine akiwemo rais Ruto katika kanisa la Emmanuel lililopo eneobunge la Makadara kaunti ya Nairobi.

Askofu alikwenda kwa ndani Zaidi na kunukuu Biblia akisema kwamba Mungu anatoa onyo kali kwa mtu yeyote ambaye anamkosea kiongozi wake heshima.

“Mtukufu rais sikuja hapa ili kukuhutubia, lakini nimesikia watu wengine wakikuita kwa njia ambayo haistahili. Wanalinganisha wewe na Zakayo, najua unajua hilo. Ni aibu. Wakristo, ni aibu, ni aibu, ni aibu. Katika kitabu cha Kutoka kifungu cha 28 mstari wake wa 32, Biblia inatupa onyo, kumtukana, kutomheshimu kiongozi wa nchi, ni sharti mjue hilo. Kazi yetu ni kumuombea na kuombea serikali.” Askofu alisema.

Askofu huyo alirejesha kumbukumbu wakati wa uchaguzi watu wengi walifurahia sana kumpata kiongozi huku akionekana kumtetea Ruto kwa tozo nyingi ili kupata hela za kuendesha nchi.

“Nakumbuka wakati wa uchaguzi, tulifurahia sana, na unajua serikali ikiingia ni ifanye kazi. Na serikali haina pesa inatoa pesa wapi? Kwetu!” askofu huyo alisema.

Hii si mara ya kwanza kwa rais Ruto kulisikia jina hilo.

Mwaka jana, alisema kwamba yeye hajali kama watu wanambandika majina hayo yote likiwemo la Zakayo, bali anachozingatia Zaidi ni kuhakikisha kila mwananchi anatoa ushuru kwa ajili ya kuendeshwa kwa serikali.

Ruto akizunumza Jumapli pia katika ibada hiyo, alisema kwamba yeye ana ndoto pevu sana juu ya Kenya, na kukanusha kuwa alichaguliwa kujaza nafasi ya rais wa nchi.

Kiongozi huyo wa nchi alisema kuwa mpango wa nyumba za bei nafuu utaendelea lakini akaweka nadhiri kwamba hakuna mwananchi atakayefurushwa kutoka sehemu ambayo nyumba hizo zitajengwa.

Ruto aliahidi kuwa serikali yake itawafidia Wakenya watakaoathirika na kuhamishwa huko kwa kuwalipia kodi ya kila mwezi kwa kipindi cha miaka 2 wakisubiria kukamilika kwa ujenzi wa nyumba za bei nafuu.