Rais wa Malawi Chakwera awasili nchini kwa ziara ya Kiserikali

Muhtasari
  • Rais wa Malawi Chakwera awasili nchini kwa ziara ya Kiserikali
Rais wa Malawi Chakwera awasili nchini kwa ziara ya Kiserikali
Image: PSCU

Rais Lazarus Chakwera wa Malawi na mkewe Monica wamewasili nchini kwa ziara ya kiserikali ya siku tatu.

Chakwera atakuwa mgeni mkuu katika sherehe za Siku ya Mashujaa ya mwaka huu ambayo itafanyika katika uwanja wa Wang'uru kaunti ya Kirinyaga Jumatano.

Ndege ya Kenya Airways iliyokuwa imebeba wawili hao iliwasili mchana huu katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta.

Walipowasili, walipokelewa na Waziri wa Ulinzi Eugene Wamalwa na mwenzake wa ICT Joe Mucheru.

Rais Uhuru Kenyatta na Mkewe Margaret Kenyatta wanatarajiwa kumpokea rais huyo anayemtembelea na ujumbe wake Alhamisi Ikulu, Nairobi.

Ni ziara ya kwanza ya Chakwera nchini kama rais baada ya kushinda uchaguzi wa mwaka jana, akimshinda Peter Mutharika kwa asilimia 58.57 ya kura.

Siku ya Mashujaa huzingatiwa mnamo Oktoba 20 kama likizo ya umma kwa pamoja kuwaheshimu wale wote waliochangia kupigania uhuru wa Kenya au walichangia vyema Kenya baada ya uhuru Kenya.

Maandalizi ya sherehe hizo yamekamilika na malango ya kuingia uwanjani yatafunguliwa kuanzia saa nne asubuhi.