Shangazi wa mtoto wa miaka 3, Junior Sagini, anayedaiwa kumng'oa macho azuiliwa

Nyakerario alilia bila kujizuia wakati upande wa mashtaka ukisoma mashtaka.

Muhtasari

•Sagini, 3, aling’olewa macho katika kinachodaiwa kuwa tambiko lililofanyika siku ya Alhamisi usiku katika eneo la Marani, Kisii.

•Pacifica atazuiliwa katika kituo cha polisi cha Rioma huku akisubiri kesi kutajwa siku ya Ijumaa tarehe 23.

JARIBIO LA MAUAJI: Pacifica Nyakerario akiongozwa nje ya mahakama ya Kisii Jumanne, Desemba 20.
JARIBIO LA MAUAJI: Pacifica Nyakerario akiongozwa nje ya mahakama ya Kisii Jumanne, Desemba 20.
Image: MAGATI OBEBO

Mshukiwa mkuu katika kesi ya Junior Sagini amezuiliwa kwa siku nne zaidi huku wapelelezi wakiendelea na uchunguzi zaidi.

Sagini, 3, aling’olewa macho katika kinachodaiwa kuwa tambiko lililofanyika siku ya Alhamisi usiku katika eneo la Marani, Kisii.

Pacifica Nyakerario ambaye alikuwa ametoweka alikamatwa Jumatatu jioni jijini Nairobi.

Alifikishwa mbele ya hakimu mkazi mkuu Christine Ongweno Jumanne asubuhi kwa mashtaka ya kujaribu kuua.

Akiwa kizimbani, Nyakerario alilia bila kujizuia wakati upande wa mashtaka ukisoma mashtaka.

Atazuiliwa katika kituo cha polisi cha Rioma huku akisubiri kesi kutajwa siku ya Ijumaa tarehe 23.

Kushtakiwa kwa Nyakerario kunajiri siku moja baada ya mshukiwa wa kwanza, ambaye ni mwanawe, Alex Ochogo, kukamatwa kwa mashtaka sawia.

Baby Sagini alishambuliwa siku ya Alhamisi baada ya kuachana na watoto wengine.

Baadaye alipatikana akiwa ametobolewa macho na akijikunja kwa maumivu.

Wakati huo huo, kulikuwa na kisa cha muda nje ya mahakama ya Kisii huku wanawake waliojitokeza kusikiliza kesi hiyo wakimshutumu mshukiwa kwa kuchafua jina la Marani na kisa hicho.

Utafsiri: Samuel Maina