Binti ya Jenerali Francis Ogolla avunja kimya kufuatia ajali ya ndege iliyomuua babake

Bi Lorna Ogolla alibainisha kuwa marehemu alifariki akifanya kazi yake bora ya kujaribu kuweka Kenya salama.

Muhtasari

•Bi Lorna A. Omondi Ogolla  ameomboleza kihisia kufuatia kifo cha cha kusikitisha cha baba yake, Jenerali Francis Ogolla.

•Lorna alimtaja babake kama mtu mchapakazi na aliyejitolea sana ambaye alikuwa kila mara kufanya mazoezi na wanajeshi wake wa KDF.

amemuomboleza baba yake Jeneral Francis Ogolla
Bi Lorna Ogolla amemuomboleza baba yake Jeneral Francis Ogolla
Image: HISANI

Bi Lorna A. Omondi Ogolla, binti ya marehemu Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ya Kenya, Jenerali Francis Ogolla ameomboleza kihisia kufuatia kifo cha cha kusikitisha cha mzazi huyo wake siku ya Alhamisi.

Jenerali Ogolla ni miongoni mwa wanajeshi kumi waliopoteza maisha katika ajali ya ndege iliyotokea Alhamisi alasiri katika eneo la Sindar, lokesheni ya Kaben, tarafa ya Tot, kaunti ya Elgeyo Marakwet.

Huku akimuomboleza babake kupitia akaunti yake ya LinkedIn, Bi Lorna Ogolla alibainisha kuwa marehemu alifariki akifanya kazi yake bora ya kujaribu kuweka Kenya salama.

"Baba yangu, mfuatiliaji wa ubora, kiongozi mwenye huruma na ufanisi zaidi na mwanaserikali alianguka kwenye ajali ya chopper iliyotokea Pokot Magharibi akifanya kile alichofanya vyema zaidi kwa kipindi cha miaka 40 iliyopita - akijaribu kuweka Kenya Salama," Bi Lorna Ogolla alisema katika taarifa ya Alhamisi jioni.

Aliongeza, “Siku moja nitasimulia hadithi nzuri za jinsi alivyofundisha kwa matendo yake na si kwa maneno yake. Lakini leo - ninakimbia nyumbani ili kumuaga kwenda kwenye ukumbi mkubwa zaidi.

Lorna pia alimtaja babake kama mtu mchapakazi na aliyejitolea sana ambaye alikuwa kila mara kufanya mazoezi na wanajeshi wake wa KDF.

“Unajua nilichokuwa nakipenda zaidi, hakuwaambia tu watu wafanye vitu, alivifanya yeye mwenyewe.. Jumanne na Ijumaa ilikuwa siku ya mazoezi na wanaume na wanawake hawa na alikuwa nje nao, hata siku za shughuli nyingi au siku za mvua,” alisema chini ya picha ya marehemu Jenerali Ogolla akifanya mazoezi na wanajeshi wenzake.

Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Francis Ogolla alikuwa miongoni mwa maafisa wa KDF waliopoteza maisha katika ajali mbaya iliyotokea katika eneo la Sindar, lokesheni ya Kaben, tarafa ya Tot, Kaunti ya Elgeyo Marakwet.

Maafisa wengine tisa walioaga dunia ni pamoja na Brig Swaleh Saidi, Kanali Duncan Keitany, Lt Kanali David Sawe, Meja George Benson Magondu (ambaye pia alikuwa rubani), Capt Sorah Mohamed, Capt Hillary Litali, Sajenti Mwandamizi John Kinywa Mureithi, Sajenti Cliffonce Omondi na Sajenti Rose Nyawira.

Kufuatia kifo cha Ogolla, Rais William Ruto alitangaza kipindi cha siku tatu cha maombolezo ya kitaifa kuanzia Ijumaa, Aprili 19, 2024.

Alisema katika kipindi hicho, bendera ya Kenya na ile ya Majeshi ya Ulinzi ya Kenya, Jumuiya ya Afrika Mashariki na bendera za makundi yote ya kijeshi zitapepea nusu mlingoti nchini Kenya na Kenya nje ya nchi.