Mwanamitindo Edwin Chiloba apatikana amekufa na mwili kuwekwa kwenye sanduku la chuma

Polisi katika kaunti ya Uasin Gishu wanajaribu kutatua mauaji hayo.

Muhtasari

•Mwili wa Chiloba ulipatikana ukiwa umewekwa kwenye sanduku la chuma katika eneo la Mogombet, eneo bunge la Kapsaret katika Kaunti ya Uasin Gishu.

alipatikana amefariki na mwili wake kuwekwa ndani ya sanduku
Mwanamitindo Edwin Chiloba alipatikana amefariki na mwili wake kuwekwa ndani ya sanduku
Image: HISANI

Mwanamitindo maarufu Edwin Chiloba amefariki dunia.

Mwili wa Chiloba ulipatikana ukiwa umewekwa kwenye sanduku la chuma katika eneo la Mogombet, eneo bunge la Kapsaret katika Kaunti ya Uasin Gishu.

Polisi katika kaunti ya Uasin Gishu wanajaribu kutatua kitendawili kilichozingira mauaji hayo.

Duru za kuaminika zinasema kwamba mwendesha Bodaboda mmoja aliona gari ambalo halikuwa na nambari ya usajili likidondosha sanduku la chuma kando ya barabara ya Kipenyo - Kaptinga.

Kesi hiyo iliripotiwa kwa polisi wa Uasin Gishu ambao walifika katika eneo la tukio na walipofungua sanduku hilo, mwili wa mwanamume aliyekuwa amevalia nguo za kike ambao ulikuwa ukioza ulipatikana ndani.

Baadaye ilibainika kuwa marehemu alikuwa mwanamitindo wa Eldoret Edwin Chiloba.

Mwili huo ulipelekwa katika Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Moi ukisubiri uchunguzi wa maiti kubaini sababu ya kifo.

Asili ya Edwin Chiloba

Edwin alizaliwa Elgeyo Marakwet, na katika mahojiano ya awali, alisema utoto wake ulijaa dhiki baada ya kumpoteza mama yake akiwa na umri mdogo sana.

Kifo kilitokea tena katika shule ya upili, na kumnyang'anya baba yake - mzazi pekee ambaye alikuwa amesalia.

Alizungumza vyema juu ya baba yake akisema kwamba alipata hisia ya kukubalika na kuwa kutoka kwa mwanaume huyo ambaye alihimiza upekee wake.

Alipata mafanikio yake kupitia ujumbe wa Facebook kutoka kwa wanandoa wazungu ambao walipenda miundo yake.

Roho yake ipumzike kwa amani.