Kinda wa Man United Kobbie Mainoo apigwa na butwaa baada ya kuitwa kuwakilisha Uingereza

Kiungo huyo alisema ni jambo ambalo bado hajaliamini kabisa kwani mambo yalifanyika kwa kasi.

Muhtasari

•Mainoo ni miongoni mwa wachezaji 25 walioitwa na kocha Gareth Southgate kuiwakilisha Uingereza katika mechi zijazo za kimataifa.

•"Sidhani kama bado imezama akilini, lakini ndio, nina furaha kwa wiki. Nyumbani, wote wamefurahi," Mainoo alisema.

ameitwa kuwakilisha Uingereza
Kobbie Mainoo ameitwa kuwakilisha Uingereza
Image: HISANI

Kiungo chipukizi wa Manchester United Kobbie Mainoo alipigwa na butwaa na kufurahi baada ya kujumuishwa katika kikosi cha Uingereza kwa mara ya kwanza.

Mwanasoka huyo mwenye umri wa miaka 18 ni miongoni mwa wachezaji 25 walioitwa na kocha Gareth Southgate kuiwakilisha Uingereza katika mechi zijazo za kimataifa.

Shirikisho la Soka la Uingereza lilithibitisha kuwepo kwake katika kikosi hicho wakati likitangaza kuwasili kwa wachezaji wote siku ya Jumanne.

“Kobbie Mainoo amepokea mwito wake wa kwanza kwenye kikosi cha wachezaji wakubwa cha wanaume cha Uingereza. Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 18 awali alikuwa sehemu ya kikosi cha MU21 lakini amejumuishwa katika kundi la Gareth Southgate,” Shirikisho la Soka la England lilisema katika taarifa.

Taarifa hiyo ilisema zaidi, "Wachezaji wengine wote 25 waliripoti St. George's Park Jumanne kabla ya mechi zijazo za kimataifa dhidi ya Brazil na Ubelgiji. Kiungo wa kati wa Manchester United Mainoo amewahi kuiwakilisha Uingereza katika MU17 hadi kiwango cha MU19.”

Mainoo amekuwa nguzo kubwa katika kikosi cha Mashetani Wekundu msimu huu baada ya kujumuishwa katika mechi nyingi ambazo klabu hiyo imecheza.

Akizungumzia kuitwa kuliwakilisha taifa lake, kiungo huyo alisema ni jambo ambalo bado hajaliamini kabisa kwani mambo yalifanyika kwa kasi.

“Niliitwa kwa vijana wa chini ya miaka 21 kisha nikapokea ujumbe kutoka kwa Steve Holland. Aliniambia nije kukutana naye kwenye eneo la mapokezi na akaniambia tu kwamba nimeitwa na nitakuwa na kikosi kwa wiki,” Mainoo alisema.

Aliongeza, "Sidhani kama bado imezama akilini, lakini ndio, nina furaha kwa wiki. Nyumbani, wote wamefurahi.”

Inaaminika kuwa mchezaji huyo chipukizi amejumuishwa kwenye kikosi cha England ili waweze kukuza kipaji chake bora.