Vijana wake Ancelotti wang'aa kama mabingwa

Vinicius Junior ateuliwa kama mchezaji wa msimu ilhali Jude Bellingham ateuliwa kama mchezaji mwenye umri mdogo katika ubingwa wa ulaya

Muhtasari
  • Vinicius Junior alikuwa na jumla ya mabao sita pamoja na kuwasaidia wenzake kufunga mabao manne.
  • Jude Bellingham aliisaidia Real Madrid kwa kufunga mabao manne na kusaidia wenzake kufunga mabao matano
mshambuliaji wa Real Madrid Vinicius Junior
Image: INSTAGRAM// VINI JR

Mshambuliaji matata wa Real Madrid Vinicius Junior ameteuliwa kuwa mchezaji bora wa msimu huu katika ligi ya mabingwa ya ulaya.

Vilevile, kiungo wa kati katika timu hiyo Jude Bellingham ameteuliwa kama mchezaji bora mwenye umri mdogo katika msimu huu.

Vinicius Junior alikuwa na jukumu azizi katika kuisaidia timu ya Real Madrid kunyakua ubingwa wa ulaya ambapo alikuwa na jumla ya mabao sita pamoja na kuwasaidia wenzake kufunga mabao manne.

Vilevile Jude Bellingham aliyeteuliwa kama mchezaji mdogo mwenye umahiri zaidi aliisaidia Real Madrid kwa kufunga mabao manne na kusaidia wenzake kufunga mabao matano.

Ama kweli, umahiri huu ulidhihirika dhahiri shahiri kwani wachezaji hawa walijitolea mhanga na kutia juhudi na jitihada kuhakikisha Real Madrid haitwai ubingwa wa ulaya tu bali pia ubingwa wa ligi kuu LALIGA.

Ama kweli, kikosi chake Carlo Ancelotti kimekuwa cha bidii na jitihada kwani ni kutokana na umahiri wa wachezaji hawa wawili hasa ambao umekua adhimu msimu huu.

Jude Bellingham alijiunga na kikosi cha Real Madrid mnamo mwaka jana kutoka kwa timu ya Borussia Dortmund ilhali Vinicius Junior alitoka kwenye timu ya Flamengo mnamo mwaka wa 2017 na kutoka hapo ameisadia timu ya Real Madrid kunyakua mataji mawili ya ubingwa wa ulaya huku akifunga mabao mawili katika fainali mbili za ubingwa wa ulaya.