Otile Brown afichua kwa nini alificha kuwa ni Mjaluo kwa muda mrefu

Brown amefichua kuwa alificha utambulisho wake wa kabila kwa muda mrefu.

Muhtasari

•Brown ambaye ni mzaliwa wa Mombasa alifichua kuwa wazazi wake wote wawili walikuwa kutoka jamii ya Wajaluo.

•Brown alidai kwamba utambulisho wake wa kabila ulijulikana baada ya kufanya shughuli ya Mpesa.

Image: RADIO JAMBO

Mwanamuziki Jacob Juma Obunga almaarufu Otile Brown  amefichua kuwa alificha utambulisho wake wa kabila kwa muda mrefu.

Akizungumza katika kipindi cha Bustani la Massawe, Brown ambaye ni mzaliwa wa Mombasa aliweka wazi kuwa wazazi wake wote wawili walitokea jamii ya Luo.

Otile hata hivyo hakujitambulisha na jamii hiyo kwa kuwa alikua miongoni mwa Waswahili na alihofia kutengwa kwa misingi ya kikabila.

“Mimi nimezaliwa Mombasa kwenye jamii ya Waswahili. Kama unavyojua kitambo kulikuwa na ukabila na mimi sikutaka kipaji changu kipunguzwe katika eneo fulani,” Otile alisema.

Mwanamuziki huyo pia alisema hakutaka kujihusisha na jamii yake kutokana na sifa ya majigambo wanayohusishwa nayo.

Brown alidai kwamba utambulisho wake wa kabila ulijulikana baadaye maishani baada ya kufanya shughuli ya Mpesa.

Alidai kuwa kuna mtu asiyejua ambaye alitangaza jina lake rasmi baada ya kufanya naye shughuli ya Mpesa.

“Nilikuwa najificha kwa sababu Wajaluo husemekana ni wenye majigambo. Kuna wakati nilituma Mpesa alafu mtu akanisema. Sikujua ni nani,” Alisema.

Brown hata hivyo aliweka wazi kuwa anailewa lugha ya Kiluo na akasema kuwa anaweza kuizungumza bila tashwishi.

Katika kipindi hicho,  Otile Brown pia alizungumza kuhusu maisha yake magumu ya utotoni baada ya wazazi wake wote kuaga.

Msanii huyo mwenye umri wa miaka 30 alifichua kuwa wazazi wote wawili walifariki akiwa na umri mdogo.

“Mama alifariki, Baba alifariki. Sikulelewa na baba, slifariki nikiwa mchanga. Mama alifariki nikiwa na miaka 12. Nililelewa na mamangu mdogo,” Alisema.

Brown alisema yeye ni mtoto wa mwisho katika familia ya watoto watano. Alifichua kuwa yeye na ndugu zake walikua katika hali ngumu baada ya wazazi wote wawili kufariki.

Pia alieleza kuwa shangazi yake na majirani ndio waliofanikisha masomo yake hadi hatua ya kidato cha nne.

Brown ambaye amebarikiwa na talanta kubwa alianza kuvuma takriban miaka mitano iliyopita na umaarufu wake umekuwa ukipanda kila uchao