Patanisho: Mwanadada amuibia dadake baada ya kukaribishwa nyumbani kwake

Maureen alichukua nguo na gesi ya dada yake kwa madai hakuwa akimlipa.

Muhtasari

•Maureen alisema uhusiano wake na dadake uliingia dosari wakati wa janga la Corona baada ya kuchukua nguo zake bila idhini.

•Benta alifichua kuwa kando na nguo zake, dadake mdogo pia alibeba mtungi wake wa gesi wakati alipotoka kwake.

Gidi Ogidi
Image: RADIO JAMBO

Katika kipindi cha Gidi na Ghost asubuhi, kitengo cha Patanisho, mwanadada aliyejitambulisha kama Maureen alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na dada yake Benta ambaye alikosana naye kufuatia mzozo wa nguo.

Maureen alisema uhusiano wake na dadake uliingia dosari wakati wa janga la Corona baada ya kuchukua nguo zake bila idhini.

"Anaishi Nakuru. Wakati wa Corona alinipigia simu akaniambia niende nimsaidie. Nilifika huko na nikaishi na yeye. Sikuwa na nguo nyingi. Dadangu ana manguo mingi. Siku moja nilikuwa nataka kuenda kuona Otile Brown, nikachukua nguo zake nikavaa," alisimulia.

"Baadae kufika wakati wa kuenda ushago ulipofika tukaanza kukosana kwa sababu hata hakuwa ananipatia pesa. Nilichukua nguo zake nikaenda nazo. Ilikuwa nguo kama nne hivi, sikumuuliza kama naweza kuzibeba," alisema.

Benta alipopigiwa simu alikuwa mchache wa maneno ila akaweka wazi kwamba amekubali ombi la msamaha la dadake.

Hata hivyo alifichua kuwa kando na nguo zake, dadake mdogo pia alibeba mtungi wake wa gesi wakati alipotoka kwake.

"Hakuniomba nguo. Alibeba hadi gas.. mimi nimeshamsamehea," alisema.

Huku akijitetea kwa kubeba gesi ya dadake, Maureen alidai kwamba kaka yao ndiye aliyemuuzia kwa pesa kidogo.

"Sikuwa najua ni yake. Nilipatia kakangu pesa kidogo na akaniambia ninyamaze," alisema.

Wawili hao walikubali kumaliza tofauti zao huku Benta akimshauri dada huyo wake abadilishe mienendo yake mibaya baada ya kumsamehe.