Gidi amkumbuka rafiki yake marehemu Fidel Odinga

Fidel alifariki mnamo Januari 4, 2015 nyumbani kwake Windy Ridge, Karen.

Muhtasari

•Mtangazaji wa Gidi na Ghost Asubuhi kwenye Radio Jambo, Gidi Ogidi amemkumbuka marehemu kama rafiki na kaka yake.

• Gidi amemtaja marehemu kama mtu aliyekuwa na moyo mzuri ambaye matendo yake bado yanakumbukwa.

Marehemu Fidel Odinga na mtangazaji Gidi Ogidi
Image: INSTAGRAM// GIDI OGIDI

Januari 4, ni siku ambapo kifo cha mwana wa kwanza wa kiongozi wa ODM Raila Odinga, Fidel Castro Obange Odinga kinaadhimishwa.

Fidel alifariki mnamo Januari 2015 nyumbani kwake Windy Ridge, Karen baada ya kujiburudisha na marafiki zake usiku uliotangulia.

Mtangazaji wa Gidi na Ghost Asubuhi kwenye Radio Jambo, Gidi Ogidi amemkumbuka marehemu kama rafiki na kaka yake.

Huku akimkumbuka, Gidi amemtaja marehemu kama mtu aliyekuwa na moyo mzuri ambaye matendo yake bado yanakumbukwa.

"Rafiki yangu Obange, Ndugu yangu Fidel, Bado tunakukumbuka. Mtu mwenye moyo mzuri ulituacha mapema lakini matendo yako yanaishi," Gidi alisema kwenye ukurasa wake wa mtandao wa Facebook.

Aliambatanisha ujumbe huo na picha yake ya kumbukumbu akiwa na Fidel kutoka siku ambazo marehemu  alikuwa hai.

"Endelea kupumzika kwa Amani kaka 🙏🏿," alisema.

Fidel ambaye alizaliwa 1973, alikuwa kwenye ndoa na mwanamke kutoka Eritrea, Getachew Bekele, ambaye walizaa naye mtoto mmoja.

Mwili wake ulipatikana kitandani chake mnamo Januari 4, 2015 asubuhi na kilichosababisha kifo hicho hakikuweza kubainika mara moja.  Alikutwa amefariki na mkewe ambaye alimpigia simu mzazi wa Fidel akiwa amejawa na hofu.

Kabla ya kifo chake, nyota ya kisiasa ya Fidel ilikuwa iking'aa na alionekana kama mrithi wa kipekee  jina la Odinga katika siasa za Kenya.

Fidel alikuwa mwana mkubwa katika familia ya watoto wanne Rosemary, Raila Junior na Winnie. Alikuwa na umri wa miaka 41 alipofariki.