"Asante kwa upendo" Harmonize amuingiza dadake Diamond kwenye muziki, asifia sauti yake

"Asante kwa upendo safi na urafiki Chima. Mungu akubariki," Harmonize alimwambia Esma.

Muhtasari

•Katika taarifa yake ya Jumamosi, Staa huyo wa  Bongo alimsifia dadake Diamond na kutaja sauti yake kama ya kupendeza.

•Pia alimshukuru dada huyo wa hasidi wake mkuu kwa kuchangia kwenye wimbo huo na kwa upendo na urafiki wao.

Harmonize, Diamond, Esma
Image: INSTAGRAM

Bosi wa Konde Music Worldwide, Rajab Abdul Kahali almaarufu Harmonize ameweka wazi kuwa dada mkubwa wa Diamond, Esma Platnumz amehusika katika wimbo wake mpya  akimshirikisha DJ Seven 'Say Yes'.

Katika taarifa yake ya Jumamosi, Konde Boy alibainisha kuwa Esma Platnumz ameweka sauti yake kwenye korasi ya wimbo huo.

Staa huyo wa  Bongo alimsifia dadake Diamond na kutaja sauti yake kama ya kupendeza.

"Eid Mubarak watu wangu wimbo wa  @djsevenworldwide ft Single Boy  & Esma #SAYYESS umetoka. Sasa sikutaka kusema hili lakini lazima nimtambue malkia. Hizo sauti za kike za chini zilizo pendezesha hapo kwenye baby kitendawili,, Tega!! Naziona Popo Mbili.. Macho Esma alifanya," aliandika kwenye Instagram.

Mwimbaji huyo wa kibao 'Single Again' alimbatanisha taarifa yake na sauti ya  sehemu ya wimbo huo mpya.

Pia alimshukuru dada huyo wa hasidi wake mkuu kwa kuchangia kwenye wimbo huo na kwa upendo na urafiki wao.

"Asante kwa upendo safi na urafiki Chima. Mungu akubariki," alisema.

Katika siku za hivi majuzi, msanii huyo wa zamani wa WCB na Esma wamebainisha kuwa kuna uhusiano mzuri kati yao. Urafiki wao hata hivyo una utata ikizingatiwa kwamba Harmonize na kakake Esma,  Diamond Platnumz wanachukuliwa kuwa mahasidi wakubwa zaidi katika tasnia ya muziki wa Bongo.

Katikati mwa mwezi Februari, video ya Esma akifurahiya wimbo mpya wa Harmonize ‘Single Again’ iilivuma kwenye mitandao ya kijamii.

Dada mkubwa huyo wa Diamond alikuwa ndani ya  gari na mwanamke mwingine alipojirekodi akiimba sehemu ya wimbo huo uliotolewa  mnamo Siku ya Wapendanao.

“Masingle lady mmeona? Mimi kila siku niko single, sijui mwenzangu. Hadi siku ya Valentine's tupo single" alisikika akisema huku wimbo huo ukiendelea kucheza kwenye redio ya gari.

Mama huyo wa watoto watatu alionekana kuufurahia sana wimbo huo na hata alisikika akiimba pia huku wimbo ukiendelea kucheza.

"I'm single. Do you know that I'm single? I'm single again! Who knows that I'm single? Ooh yes, I'm single. Ladies I'm single again!I 'm single. Who knows I'm single?"  aliimba.

Hatua ya Esma ya kuimba wimbo wa Harmonize ilizua gumzo ikizingatiwa kuwa bosi huyo wa Kondegang ni hasidi nambari moja wa kaka yake, Diamond Platnumz.