Akuku Danger avunja kimya baada ya kuzidiwa na ugonjwa hadi kulazwa hospitali

Mchekeshaji huyo aligundulika kuwa na ugonjwa huo wa wa kurithi akiwa na umri wa miaka saba.

Muhtasari

•Akuku Danger alisema anaendelea kupata nafuu nyumbani baada ya kuruhusiwa kutoka hospitalini alikokuwa amelazwa kwa siku kadhaa.

•Mchekeshaji huyo aliwashukuru mashabiki wake kwa jumbe za kutia moyo walizomtumia baada ya kujua kuhusu ugonjwa wake.

Image: INSTAGRAM// AKUKU DANGER

Mchekeshaji mashuhuri wa Kenya Mannerson Oduor Ochieng almaarufu Akuku Danger mnamo siku ya Jumatatu alifichua kwamba kwa sasa anaendelea kupata nafuu nyumbani baada ya kuruhusiwa kutoka hospitalini alikokuwa amelazwa kwa siku kadhaa ambazo hajafichua.

Katika taarifa yake kwenye mtandao wa Instagram, mchekeshaji huyo wa zamani wa Churchill Show ambaye amekuwa akipambana na ugonjwa wa anemia ya seli mundu kwa miaka mingi alidokeza kuwa hajakuwa sawa kiafya katika wiki kadhaa zilizopita.

Alizungumza kuhusu makaliya ugonjwa huo ambao aligunduliwa kuwa nao akiwa mtoto lakini akafichua kuwa sasa anaendelea vizuri baada ya kuruhusiwa kutoka hospitalini.

“Wiki Hizi Chache Zilizopita, Mungu amekuja Kwa Ajili Yangu. Sickle Cell Ni Ugonjwa Mbaya😓. Dakika Moja Unaendelea na biashara yako na kufanya bidii kukimbiza begi hii na dakika inayofuata unapigania maisha yako hospitalini,” Akuku Danger alisema siku ya  Jumatatu.

Aliambatanisha taarifa yake na video ambayo ilimuonyesha akiwa amelala kwenye kitanda cha hospitali na kifaa cha hewa mdomoni na puani.

“Siandiki i haya kwa ajili ya kuhurumiwa au chochote bali kwa ajili ya wapiganaji wote wa seli mundu huko nje ambao wanatafuta maongozi na Ndiyo! WOTE MNA NGUVU KULIKO MNAVYOWAZA!!❤️❤️. Tumerudi Sasa!! Yote ni nzuri na nje ya hospitali. Tuendelee na Kazi,” aliongeza.

Katika taarifa nyingine Jumatatu jioni, mchekeshaji huyo aliwashukuru mashabiki wake kwa jumbe za kutia moyo walizomtumia baada ya kujua kuhusu ugonjwa wake.

Aliendelea kuwahakikishia mashabiki wake kuwa anaendelea vyema zaidi. Pia alitumia fursa hiyo kuwatia moyo watu wengine wanaopambana na anemia ya seli mundu.

“Asanteni nyote kwa jumbe zenu za kutia moyo. Tayari niko nje ya hatari, napata nafuu tu kutoka nyumbani. Kwa walezi, wazazi kwa wanaopambana na seli mundu na wapambanaji wenyewe, weka imani thabiti,” Akuku Danger alisema.

Aliongeza, “Tutashinda siku moja. Maumivu tunayopata kutokana na majanga haya chungu ni wewe tu unaweza kuyasikia. Hata hivyo tunaendelea kuwa askari.”

Akuku Danger amekuwa akipambana na ugonjwa wa anemia ya seli mundu kwa miaka mingi baada ya kugundulika kuwa na ugonjwa huo wa wa kurithi akiwa na umri wa miaka saba.