"Ni bonasi!" Guardian Angel azungumza kuhusu kupata mtoto na mkewe Esther Musila

Muhtasari

•Guardian Angel alisema kwamba kupata mtoto na Bi Musila ni bonasi kutoka kwa Mungu  ambayo kwake si sharti wapate.

• Musila aliwasuta wale ambao wamekuwa wakifuatilia kujua kuhusu mpango wao wa kupata watoto.

Esther Musila na mumewe Guardian Angel
Esther Musila na mumewe Guardian Angel
Image: INSTAGRAM//GUARDIAN ANGEL

Mwimbaji wa nyimbo za injili Peter Omwaka almaarufu Guardian Angel ameweka wazi kuwa kupata watoto sio kipaumbele kikuu katika ndoa yake na Esther Musila.

Katika mahojiano, mwanamuziki huyo mwenye umri wa miaka 32 alisema kipaumbele cha mahusiano yao ni mapenzi.

Guardian Angel alisema kwamba kupata mtoto na Bi Musila ni bonasi kutoka kwa Mungu  ambayo kwake si sharti wapate.

"Nilipoingia kwenye ndoa yetu, mtoto ni nambari mbili. Akija ama akose ni sawa. Nambari moja ni upendo wetu. Mungu akitaka kutupatia bonasi ya baraka ya mtoto ni sawa. Lakini kama haipo, hiyo ni bonasi, tunafurahia na tulicho nacho. Upendo wetu ndio ninaojali," Guardian Angel alisema katika mahojiano na Plug TV.

Mwanamuziki huyo alisema upendo wao pekee umetosha na kueleza kuwa umemletea amani kubwa moyoni.

"Tukipata mtoto ni sawa, tukikosa pia haipunguzi chochote kwa upendo wangu kwa mke wangu," Alisema.

Kwa upande wake Musila aliwasuta wale ambao wamekuwa wakifuatilia kujua kuhusu mpango wao wa kupata watoto.

Alibainisha kuwa suala la kupata mtoto ni kati yake na mumewe.

"Mtoto ata kama hatupati, si ni wetu? sio wa jamii! Mtoto mnataka mfanyie nini na ni wetu," Musila alihoji.

Wanandoa hao walifunga pingu za maisha Januari mwaka huu baada ya kuchumbiana kwa zaidi ya mwaka mmoja.

Guardian ameweka wazi kuwa aliamua kumuoa Musila kwani alikuwa na uhakika kuwa ndiye chaguo lake la mke.

"Sikuwa na shaka yoyote. Nilijua ni uamuzi wangu. Nilijua amefanya nihisi jinsi ambavyo sijawahi kuhisi na mwingine. Ulikuwa uamuzi wangu," Alisema.

Mwanamuziki huyo pia alifichua kuwa yeye ndiye aliyependekeza mahusiano kati yake na Bi Musila.

Musila hata hivyo alikiri kuwa mwanzoni alitilia shaka mahusiano hayo kwani alihofia kile ambacho jamii ingesema.

Wakenya walitoa hisia mseto wakati wawili hao walianza kuchumbuiana, baadhi wakiwasuta kutokana na utofauti mkubwa kati ya umri wao huku wengine wakiunga mkono uamuzi wao.