Jimal Rohosafi alazwa hospitalini baada ya kuugua ghafla

Jimal alidokeza kuwa alilazwa mwendo wa saa saba usiku.

Muhtasari

•Mfanyibiashara huyo alifichua kwamba alianza kuugua muda mfupi tu baada ya kuondoka ofisini mwake.

•Haya yanajiri takriban wiki mbili baada ya kuanzisha juhudi za kufufua ndoa yake iliyosambaratika.

Mfanyabiashara Jimal Rohosafi akionekana mwenye mawazo tumbi nzima
Mfanyabiashara Jimal Rohosafi akionekana mwenye mawazo tumbi nzima
Image: Instagram//JimalRohosafi

Mwenyekiti wa muungano wa wamiliki matatu jijini Nairobi Jimal Rohosafi anaendelea kupokea matibabu hospitali baada ya kulazwa.

Jimal alitangaza habari za kulazwa kwake usiku wa kuamkia Jumatatu kupitia ukurasa wake wa Instagram.

Katika chapisho lake, baba huyo wa watoto wawili alifichua kwamba alianza kuugua muda mfupi tu baada ya kuondoka ofisini mwake.

"Nachukia hospitali.. sekunde chache tu baada ya kutoka ofisini.. Nilihisi kuwa siko sawa, kila kitu kitakuwa sawa," Jimal aliandika kwenye Instastori zake.

Mfanyibiashara huyo aliambatanisha ujumbe wake na picha iliyoonyesha akiwa amelala kwenye kitanda cha hospitali. Alidokeza kuwa alilazwa mwendo wa saa saba usiku. 

Jimal hata hivyo hakutoa maelezo zaidi wala kufichua ugonjwa unaomuathiri hadi kufikia kulazwa.

Haya yanajiri takriban wiki mbili tu baada ya mfanyibiashara huyo kuanzisha juhudi za kufufua ndoa yake iliyosambaratika.

Kupitia ujumbe mrefu ambao alipakia kwenye Instagram, Jimal alikiri kuwa alimkosea sana mke wake Amira kwa kuingiza drama nyingi kwenye ndoa yao ya miaka mingi na kumuomba msamaha.

"Naomba radhi kwa kukukosea heshima, kukuaibisha, kwa kukuumiza, kwa maumivu yote na kwa huzuni niliyokuletea. 💔Samahani kwa nyakati zote ambazo sijawa mwanaume niliyeahidi kuwa," Aliandika.

Jimal alimuomba mkewe kupokea ombi lake la msamaha huku akimkumbusha jinsi ambavyo wamepitia mengi pamoja.

"Ilikuwa mbaya kabisa. Huenda nilionekana kama mtu asiye na wasiwasi lakini sikuwa na la kufanya. Nilijua haikuwa sawa, nilijua unaumia lakini sikuweza kujikusanya!Amira nafanya hivi kwa sababu ukosefu wa heshima pia ulikuwa mkubwa. Naomba radhi kwa kukosa heshima," Aliandika.

Huku akimjibu baba huyo wa watoto wake wawili, Amira alieleza kuwa hangeweza kuuelewa msamaha wa mumewe kwa wakati huo kwani ulifufua kumbukumbu ya siku mbaya za nyuma.

"Ombi hilo la msamaha limenirudisha katika sehemu moja ya giza ambayo nimewahi kuwa katika maisha yangu kwa sababu nimetafakari juu ya mengi yaliyotokea hadharani na nyuma ya milango iliyofungwa na imezua hisia nyingi," Amira alijibu.

Aidha aliomba neema ya Mungu anapoendelea kutafakari suala hilo na kueleza kuwa kwa sasa amezidiwa na hisia.

"Vidonda vingine haviponi, lazima ujifunze jinsi ya kuishi navyo," Aliandika.