Babake Diamond afunguka kuhusu kugunduliwa na saratani ya ngozi

Mzee Abdul alieleza kuwa alifanyiwa vipimo vya kidaktari baada ya mguu wake wa kulia kuugua.

Muhtasari

•Baada ya kugunduliwa kuwa na saratani, babake Diamond alipatiwa dawa za kudhibiti hali yake na madaktari wakamshauri kutafuta matibabu zaidi.

•Abdul alidokeza kuwa kabla ya kutengwa na Mamake Diamond, bosi huyo wa WCB alikuwa amejitolea kumsaidia kutafuta matibabu.

Diamond Platnumz, Mzee Abdul Juma Isack
Image: HISANI

Mjasiriamali wa Tanzania Mzee Abdul Juma Isack amefichua kuwa aligunduliwa kuwa na ugonjwa wa saratani ya ngozi.

Katika mahojiano na Matukio Amani kwenye Simulizi Na Sauti, Mzee Abdul ambaye anaaminika kuwa baba mzazi wa staa wa Bongo Diamond Platnumz alieleza kuwa alifanyiwa vipimo vya kidaktari baada ya mguu wake wa kulia kuugua.

"Ulianza mguu wa kulia. Nilikuwa nasikia ukiwashawasha. Nikaja nikafuatilia. Mara nikasikia kama sehemu inatoka maji. Nikaja kufuatilia zaidi ikiwa inatoka usaha. Ukaja kutoka mguu wa kulia na kuhamia huu mwingine. Kufutilia hospitalini wakakata ngozi kucheki wakaniambia niko na tatizo la kansa ya ngozi," Mzee Abdul alisimulia.

Alibainisha kuwa tatizo linalomuathiri lilianza katika ukubwani wake.

Baada ya kugunduliwa kuwa na saratani, babake Diamond alipatiwa dawa za kudhibiti hali yake na madaktari wakamshauri kutafuta matibabu zaidi.

"Hospitali nilikokuwa nikienda ilikuwa ni sawa. Huko nilikoenda wakanitibu kwa dawa za kienyeji mpaka navaa viatu nikawa sawa. Ila tatizo likawa kwamba naenda alafu linanirudia. Sijajua tatizo ni nini. Limekuwa tatizo la kujirudia," Alisema.

Mjasiriamali huyo alisema kuwa bintiye Zubeida ambaye anaishi Marekani ndiye aliyefanikisha matibabu yake na akamshukuru kwa hilo.

Hata hivyo ametoa wito kwa wasamaria wema kujitolea kumsaidia huku akibainisha kuwa ameshauriwa kutafuta matibabu nje ya nchi.

"Kama kuna mtaalam wa matatizo ya miguu ambaye anaweza kunisaidia, tunaweza tukakutana na kuonana niweze kupata afya njema," Alisema.

Abdul alidokeza kuwa kabla ya kutengwa na Mamake Diamond, bosi huyo wa WCB alikuwa amejitolea kumsaidia kutafuta matibabu.

"Familia niliyokua nayo ya kwanza waliniambia watanipeleka nje. nIlikua nilishakua na imanani lakini bahati mbaya ilikua sio riziki. Ikatokea tofauti." 

Kwa muda mrefu, Mzee Abdul alijulikana kama baba yake Diamond lakini mwaka wa 2021, mama ya mwimbaji alimkana na kudai kuwa mzazi mwenza wake halisi ni Mzee Nyange na si Mzee Abdul.