Trio Mio afunguka kuhusu masomo mawili yaliyompa wakati mgumu katika KCSE

Alifichua kwamba atafanya kozi ya Ubunifu wa picha na utengenezaji wa Muziki katika chuo kikuu.

Muhtasari

•Mwimbaji huyo alitaja kuwa Hisabati na Kemia hazikuwa kikombe chake cha chai na alihangaika sana katika chumba cha mtihani na mbili hizo.

•Mwimbaji huyo alikataa kuweka hadharani matokeo yake ya KCSE, akisema atafanya hivyo kwa wakati ufaao.

Image: INSTAGRAM// TRIO MIO

Rapa mdogo Trio Mio amefichua masomo mawili yaliyompa wakati mgumu wakati wa mtihani wa KCSE wa 2022.

Katika mahojiano na Jalang’o, mwimbaji huyo wa kibao ‘Achia’ alitaja kuwa Hisabati na Kemia hazikuwa kikombe chake cha chai na alihangaika sana katika chumba cha mtihani na mbili hizo.

"Kwanza hio prac (practical), buda nlikua nacheki wasee wanamove nashanga wanaenda wapi bro. Wanamove wanaenda pale hivyo kwa gas, suijui wanadu nini... bro come on munadu?" Trio Mio alisema.

Wakati huo huo, Trio alifichua kwamba atafanya kozi ya Ubunifu wa picha na utengenezaji wa Muziki katika chuo kikuu.

"Kwa sasa ninarejea shuleni na nitajitosa katika Ubunifu wa Picha na utayarishaji wa Muziki ambayo tayari ni kazi yangu - kitu ambacho napenda kufanya na kinaniingizia pesa.

"Utayarishaji wa muziki uko hivyo na watu kama Boutross wananitia moyo sana," Trio Mio alisema.

Hata hivyo, mwimbaji huyo alikataa kuweka hadharani matokeo yake ya KCSE, akisema atafanya hivyo kwa wakati ufaao.

"Wakati ukifika nitawaambia lakini sasa hivi tuzingatie muziki…," Mio aliongeza.

Wakati wa mahojiano, rapper huyo pia alizungumzia unyanyasaji wa mitandaoni dhidi yake - akifichua memes na matusi ambayo yalimgusa zaidi.

“Kuna mtu alisema muziki wangu unavuma zaidi ya muziki wake… na wengine walisema nimepata D.Ilinifanya nifikirie ikiwa ninafaa kuboresha muziki wangu au nini lakini wakati huohuo ilinipa changamoto ya kufanya vyema zaidi,” Trio Mio alieleza.

Trio pia alitaja idadi nzuri ya majina ya mastaa ambao wanamtia moyo; Khaligraph Jones, Nadia Mukami, na Savara akiwa na collabo ya ndoto yake ya kimataifa akiwa na Zinoleesky wa Nigeria.

Ufichuzi wa Trio Mio kuhusu taaluma atakayofuata unakuja baada ya kutolewa kwa matokeo ya KCSE 2022 na Waziri wa Elimu Ezekiel Machogu.

"Hongera watahiniwa wote wanaopokea matokeo leo. Sote tulijitahidi kufikia hatua hii muhimu. Ndo life inaanza na nawatakia kismat katika yote mnayokusudia kufanya baadae💯❤️," Trio alishiriki.

Wakati uo huo, mamake Trio alipuuzilia mbali madai kuwa mwanawe alipata alama ya D katika matokeo ya hivi majuzi ya KCSE.

"Kooo Sasa Sitapumua juu matokeo ya KCSE yametoka?? Tulieni. Kijana alijitahidi na ninajivunia sana. Na wale wanaobashiri D ….poleni!" alisema