KFCB yapiga marufuku wimbo wa ‘Ninyanduwe’ wa Embarambamba na ‘Niko Uchi’ wa Gettumbe

Bodi ya Uainishaji wa Filamu nchini (KFCB) imetishia hatua za kisheria dhidi ya wasanii wa humu nchini Chris Embarambamba na William Getombe

Muhtasari
  • Wasanii hao wamechunguzwa kwa matoleo yao ya hivi punde ambayo mamlaka imepiga marufuku baada ya kuonekana kuwa hayafai kwa matumizi ya umma, haswa kwa watoto.
Embarambamba na Gettumbe
Image: Hisani

Bodi ya Uainishaji wa Filamu nchini (KFCB) imetishia hatua za kisheria dhidi ya wasanii wa humu nchini Chris Embarambamba na William Getombe kutokana na kuenea kwa maudhui yasiyofaa kwenye mitandao mbalimbali ya habari.

Wasanii hao wamechunguzwa kwa matoleo yao ya hivi punde ambayo mamlaka imepiga marufuku baada ya kuonekana kuwa hayafai kwa matumizi ya umma, haswa kwa watoto.

Wimbo wa Chris Embarambamba unaoitwa "Niko Uchi" umezua mijadala kwa mada yake ya injili, ambayo KFCB inahoji kuwa inakaribisha dhihaka kwa dini ya Kikristo. Zaidi ya hayo, wimbo huo unaripotiwa kuwa na uchi, uchafu na unakuza tabia za vurugu na za kuiga, hivyo basi kuibua wasiwasi kuhusu athari zake kwa hadhira inayoweza kuguswa, hasa watoto.

Vile vile, wimbo wa William Getumbe "Yesu Ninyandue" umekosolewa kwa asili yake ya kufuru na uwezekano wa kukera hisia za kidini.

Katika taarifa iliyotolewa Jumatano, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa KFCB Nelly Muluka alitaja kazi za Embarambamba na Getombe kuwa zinakiuka Sheria ya Filamu na Michezo ya Jukwaani Sura ya 222 ya Sheria za Kenya, ambayo inaamuru kuchunguzwa na kuidhinishwa kwa maudhui yote kabla ya kusambazwa kwa umma au maonyesho.

"Wimbo unaoitwa: 'Niko Uchi', ambao unadaiwa kuwa injili unakaribisha kejeli kwa dini ya Kikristo, pia una uchi, uchafu. Aidha imebainika kuwa baadhi ya staili za uchezaji wa msanii huyo ni za kijeuri na nyingine zinaonyesha tabia ya kuiga, ambayo ikiigwa na watoto wadogo inaweza kuwa hatari na kuleta maafa,” alisema  Nelly Muluka.

Katika kujibu hoja hizo, KFCB imetoa barua za madai kwa Chris Embarambamba na William Getombe, kuwaagiza kuondoa maudhui yoyote yasiyofaa kwenye majukwaa yao. Kukosa kutii maagizo haya kunaweza kusababisha athari za kisheria, kama ilivyobainishwa na Sheria ya Filamu na Michezo ya Jukwaani Sura ya 222.

"Barua ya madai imetolewa kwa (Chris Embarambamba na William Getombe) kufuta maudhui yoyote yasiyofaa kutoka kwenye majukwaa yao mbalimbali yakishindwa, watakabiliwa na sheria kwa mujibu wa Sheria ya Filamu na Michezo ya Jukwaani Sura ya 222 ya Sheria za Kenya. ,” ilisema KFCB.

Zaidi ya hayo, KFCB imefikia majukwaa husika ya vyombo vya habari, na kuwataka kuondoa nyenzo zinazozozaniwa na wasanii waliotajwa.

"Barua zimetolewa kwa majukwaa husika ili kuondoa maudhui yasiyofaa ya Chris Embarambamba na William Getombe," aliongeza KFCB.

Wakati huo huo, Mkurugenzi Mtendaji wa KFCB anasema bodi inasalia macho katika juhudi zake za kuhakikisha utiifu wa kanuni zilizowekwa na kukuza uundaji wa maudhui unaowajibika ndani ya tasnia ya ubunifu ya Kenya.