“Kama ningekufa leo watu wangesema nimekufa vile nilitenda dhambi” - Pasta Kanyari

“Na watu wasizoee kuongea ubaya wa watu. Yaani watu wanaongea vibaya mpaka kwa mtu ambaye amekufa, najua kama ni mimi ningekuwa nimekufa leo, watu wote wangesema ‘vile ambavyo amekuwa akifanya dhambi ndivyo amekufa’."

Muhtasari

• Kanyari pia aliwatahadharisha watumizi wa mitandao ya kijamii kutokuwa na haraka kukejeli kwa kauli mbaya watumishi wa Mungu baada ya kufa.

Mchungaji wa kanisa la Salvation Healing Ministry, Victor Kanyari amevunja kimya chake kufuatia kifo cha mchungaji mwenza mwanzilishi wa kanisa la Jubilee Christian Church, JCC, Askofu Allan Kiuna.

Kiuna alifariki mapema Jumanne baada ya vita vya muda mrefu na nduli ya saratani.

Kanyari ambaye alifikiwa na taarifa hizo akiwa mjini Nakuru alifanya video akiifariji familia ya Kiuna ikiongozwa na mkewe, Kathy Kiuna pamoja na jamii nzima ya JCC.

Kanyari pia aliwatahadharisha watumizi wa mitandao ya kijamii kutokuwa na haraka kukejeli kwa kauli mbaya watumishi wa Mungu baada ya kufa.

“Naambiwa pasta Allan Kiuna hayupo nasi tena, Kiuna amefariki leo na ugonjwa wa kansa, naisikitikia familia yake, Mungu awafariji,” Kanyari alisema.

Mchungaji huyo mwenye utata alisonga mbele na kudai kwamba angekuwa ni yeye alifariki, wengi wangezungumza kwenye mitandao ya kijamii wakihusisha kifo chake na jinsi alivyokuwa anaishi.

“Na watu wasizoee kuongea ubaya wa watu. Yaani watu wanaongea vibaya mpaka kwa mtu ambaye amekufa, najua kama ni mimi ningekuwa nimekufa leo, watu wote wangesema ‘vile ambavyo amekuwa akifanya dhambi ndivyo amekufa’. Najua kama ningekufa, watu wangeongea,” Kanyari alisema.

Kufuatia kifo cha askofu Kiuna, familia yake iliomba kupatiwa muda wa faragha wakati wanapomuomboleza mpendwa wao.