Mlipuko wa Ebola katika nchi jirani ya Uganda, mgonjwa mmoja afariki

Uganda imethibitisha kuzuka kwa ugonjwa hatari wa Ebola.

Muhtasari

•Mwanaume mwenye umri wa miaka 24 anaripotiwa kufariki baada ya kupimwa na kupatikana na ugonjwa huo.

Virusi vya Ebola
Image: HISANI// WIKIPEDIA

Nchi jirani ya Uganda imethibitisha kuzuka kwa ugonjwa hatari wa Ebola.

Wizara ya afya ya Uganda imetangaza kuwa ugonjwa huo umeibuka katika Wilaya ya Mubende huku kisa kimoja kikiwa kimethibitishwa.

Mwanaume mwenye umri wa miaka 24 anaripotiwa kufariki baada ya kupimwa na kupatikana na ugonjwa huo.

"Uganda yathibitisha kuzuka kwa Ugonjwa wa Virusi vya Ebola (EVD) katika Wilaya ya Mubende, Uganda," taarifa iliyotolewa na Wizara ya Afya ya Uganda Jumanne asubuhi ilisoma.

"Kisa kilichothibitishwa ni mwanamume mwenye umri wa miaka 24 mkazi wa kijiji cha Ngabano katika Kaunti Ndogo ya Madudu wilayani Mubende aliyekuwa na dalili za EVD na baadaye kufariki dunia,"

Mwezi uliopita, Kenya iliwatahadharisha maafisa wa afya katika mpaka baada ya WHO kusema kuwa inachunguza kisa kinachoshukiwa kuwa na Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Wizara ya Afya ya Kenya tangu hapo, iliwataka maafisa wa ufuatiliaji wa afya kwenye mipaka kuwa waangalifu zaidi.

Mgonjwa huyo wa DRC alipokea huduma katika hospitali kwa maradhi mengine, lakini baadaye, akaonyesha dalili zinazoambatana na ugonjwa wa virusi vya Ebola. DRC ilitangaza mwisho wa mlipuko wake wa Ebola mwezi Juni mwaka huu.

Shirika la Afya Ulimwenguni lilisema wafanyikazi wake wanafanya kazi na mamlaka za afya kubaini mtu yeyote ambaye aliwasiliana na mwathiriwa aliyeshukiwa kuwa na Ebole  na kufuatilia afya zao.

Ebola ni ugonjwa hatari na ambao mara nyingi huwa na athari mbaya sana unaosababishwa na virusi vya Ebola.

Milipuko ya awali ya Ebola na majibu yameonyesha kuwa utambuzi wa mapema na matibabu kwa usaidizi ulioboreshwa huokoa maisha kwa kiasi kikubwa.