Hata katika ndoto zangu, Nairobi bado ni yangu - Muhoozi, mtoto wa rais Museveni

Mkuu huyo wa majeshi ya nchi kavu ya Uganda alisema kuwa ana uwezo wa kushinda uchaguzi wowote Kenya.

Muhtasari

• "Mtaa wangu wa zamani huko Westlands utakuwa nyumbani kwangu." - Muhoozi alisema.

Kainerugaba asema Tweet zake ziliwatia woga sana Wakenya
Kainerugaba asema Tweet zake ziliwatia woga sana Wakenya
Image: Tweeter

Jenerali Muhoozi Kainerugaba, mtoto wa rais wa muda mrefu wa Uganda ameendelea kusisitiza kuhusu azma yake ya kuliteka jiji la Nairobi siku moja – kauli ambayo aliitoa mwaka jana na kuzua tafrani kwenye mtandao wa Twitter.

Muhoozi kupitia ukurasa wake wa twitter mapema Jumatatu, alidokeza kwamba bado hata katika ndoto zake, analiona jiji la Nairobi likiwa kiganjani mwake na kusisitiza kwamab ndoto yake ya kuishi eneo la Westlands bado ipo hai.

“Hata katika ndoto zangu Nairobi ni yangu. Mtaa wangu wa zamani huko Westlands utakuwa nyumbani kwangu. Jiji na nchi hiyo ni yangu!” Muhoozi aliandika.

Pia aliradidi kuwa akitaka kuwania uchaguzi katika wadhifa wowote nchini Kenya anaibuka mshindi mapema asubuhi kwa kile alitaja kuwa ni mapenzi ya dhati kutoka kwa Wakenya ambao wanazikubali falsafa zake.

“Nina uwezo wa kushinda uchaguzi wowote nchini Kenya, watu wananipenda,” alisema.

Miezi michache kuelekea kukamilika kwa mwaka jana, Jenerali Muhoozi aliibua ukakasi mkubwa kwenye mitandao ya kijamii alipoandika kwamba haitamchukua Zaidi ya wiki mbili kuliteka jiji la Nairobi kwa kutumia majeshi ya UPDF ya Uganda.

Alisema kwamba kinyume na Urusi ambao wameshindwa kuiteka Ukraine kwa Zaidi yam waka mmoja sasa, kwake kuiteka Kenya ni rahisi kama kumumunya pipi tu!

Wakenya walionekana kutofurahishwa na matamshi hayo kwenye mtandao wa Twitter ambapo walimshambulia vikali kwa maneno ya kejeli, baadhi wakidadisi kuwa kauli za kiholela kama hizo zingechafua Amani ya kidiplomasia baina ya mataifa haya mawili.

Wiki kadhaa baadae, Kainerugaba alikiri kukosa na kuomba samahani kwa Wakenya akisema kuwa alikuwa anawatania tu, lakini bado anaonekana kuradidi kauli ya kuliteka jiji la Nairobi kwa kishindo.