Fuatilieni hukumu ya kesi ya urais kutoka nyumbani! Polisi wawaagiza Wakenya

Timu ya Azimio ikiongozwa na Winnie Odinga ilikuwa imewaalika wafuasi wa muungano huo kwa maandamano ya amani.

Muhtasari

•Kaimu IG wa Polisi Noor Gabow alishauri dhidi ya kukusanyika nje ya majengo ya mahakama katika mtaa wa Milimani, jijini Nairobi.

•"Maafisa wa polisi wa trafiki watatumwa vya kutosha ili kuelekeza trafiki kuzunguka kituo cha mahakama," Gabow alisema.

Benchi la majaji saba likiongozwa na Jaji Mkuu Martha Koome, naibu CJ Lady Justice Philomena Mwilu, Jaji Mohammed Ibrahim, Jaji Dkt. Smokin Wanjala, Lady Justice Njoki Ndungu, Jaji Isaac Lenaola na Jaji William Ouko wakati wa kongamano la kesi kabla ya kuanza kwa ombi la urais katika Mahakama ya Juu Agosti 30, 2022.
Image: DOUGLAS OKIDDY

Polisi wamewashauri Wakenya kufuatilia kesi wakiwa nyumbani wakati Mahakama ya Upeo itakapokuwa ikitoa uamuzi wake kuhusu kesi ya urais siku ya Jumatatu.

Katika taarifa yake Jumamosi, kaimu Inspekta Jenerali wa Polisi Noor Gabow alishauri dhidi ya kukusanyika nje ya majengo ya mahakama katika mtaa wa Milimani, jijini Nairobi.

"Tunataka kushauri umma kwa ujumla kuepuka kukusanyika katika Mahakama ya Upeo wakati wa uamuzi, au kuwa katika mikusanyiko ya watu lakini wafuate kesi kutoka kwa starehe ya nyumba zao," Gabow alisema.

Aidha, kaimu Inspekta Jenerali alisema maeneo ya mahakama yatadhibitiwa kwa matumizi ya umma na barabara zote zinazoelekea katika Mahakama ya Upeo zitafungwa.

"Maafisa wa polisi wa trafiki watatumwa vya kutosha ili kuelekeza trafiki kuzunguka kituo cha mahakama," alisema.

ambaye amechukua usukani.
Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Noor Gabow ambaye amechukua usukani.
Image: HISANI

Mnamo Agosti 22, wafuasi wa Azimio la Umoja walizingira eneo la mahakama huku kiongozi wa muungano huo Raila Odinga akiwasilisha rufaa yake. 

Wafuasi wa mwanasiasa huyo mkongwe walipiga kambi nje ya mahakama kwa saa kadhaa huku Raila na timu yake wakiwasilisha lori la ushahidi katika mahakama hiyo.

Siku ya Jumamosi timu ya Azimio ikiongozwa na bintiye Raila, Winnie Odinga ilikuwa imewaalika wafuasi wa muungano huo kwa maandamano ya amani kwenye vituo vya miji yote kwa heshima ya safari yao ya kutafuta haki. Jumbe hizo za mwaliko hata hivyo zilifutwa baadae kufuatia shinikiz la wanamitandao.

Mahakama itatoa uamuzi wake kuhusu kesi hiyo Jumatatu, Septemba 5, 2022 baada ya kukamilika kwa kusikilizwa kwa siku tatu siku ya Ijumaa.