Magari milioni 10 yametumia Expressway tangu kuzinduliwa miezi 6 iliyopita

Moja Expressway itaendesha barabara hiyo ya ushuru kwa miaka 27 kabla ya kuikabidhi kwa KeNHA.

Muhtasari

• Hata hivyo, haijabainika mara moja ikiwa nambari iliyotajwa inathibitisha magari ya kipekee au ni hesabu ya jumla ya mipito.

Barabara kuu ya Expressway jijini Nairobi, Kenya
Barabara kuu ya Expressway jijini Nairobi, Kenya
Image: The Star//Maktaba

Takriban magari milioni 10 yametumia Barabara ya Nairobi Expressway miezi sita baada ya barabara hiyo ya kilomita 27.4 kuzinduliwa kwa matumizi miezi 6 iliyopita.

Shirika la Barabara na Madaraja la China (CRBC) lilijenga barabara kuu ya ghorofa mbili kwa kutumia fedha za kibinafsi ambazo zitarejeshwa kupitia ushuru na kampuni yake tanzu, Moja Expressway, ambayo itaendesha barabara hiyo kwa miaka 27, jarida la kibiashara liliripoti.

Barabara hiyo ya mwendokasi ya Shilingi bilioni 88 inayounganisha Mlolongo na barabara kuu ya Nairobi-Nakuru kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) ilizinduliwa Julai 31, mwaka jana, na Rais mstaafu Uhuru Kenyatta.

Akizungumza wakati wa hafla ya kuadhimisha hatua ya milioni 10 Jumanne katika kituo cha Westlands, Mkurugenzi Mtendaji wa Moja Expressway Steve Zhao alibainisha kuwa, kwa wastani, magari yapatayo 50,000 hutumia barabara hiyo ya ushuru kila siku.

"Kufikia Februari 7, 2023, jumla ya magari ambayo yametumia Barabara ya Nairobi Expressway ni 10,000,000," alinukuliwa Bw Zhao.

Hata hivyo, haijabainika mara moja ikiwa nambari iliyotajwa inathibitisha magari ya kipekee au ni hesabu ya jumla ya mipito.

Wenye magari hulipa kati ya Shilingi 120 na Shilingi 1,800 wakati wa kutoka, kulingana na ukubwa wa gari na umbali unaotumika.

Barabara ya Nairobi Expressway ni mojawapo ya ushirikiano wa sekta ya umma na binafsi.

Moja Expressway itaendesha barabara hiyo ya ushuru kwa miaka 27 kabla ya kuikabidhi kwa Mamlaka ya Barabara Kuu ya Kenya (KeNHA).