COTU yajitenga na maandamano ya Jumatatu, yawataka wafanyikazi kutotii wito wa Odinga

"Tunawaomba wafanyakazi wajizuie kushiriki katika shughuli zozote zinazoweza kuhatarisha hali yao ya ajira."

Muhtasari

• Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Opiyo Wandayi alitoa wito kwa waajiri kuwaachilia wafanyikazi wao ili kushiriki katika shughuli hiyo kubwa.

Wafuasi wa Azimio wanapeperusha mabango wakati wa maandamano mjini Mombasa Jumapili, Machi 12.
Wafuasi wa Azimio wanapeperusha mabango wakati wa maandamano mjini Mombasa Jumapili, Machi 12.
Image: Twitter//Raila Odinga

Muungano wa Vyama vya Wafanyakazi (COTU) umeelezea wasiwasi wake kuhusu wito wa kinara wa upinzani Raila Odinga wa kuchukua hatua ya maandamano kupinga gharama ya juu ya maisha.

Katika taarifa iliyotolewa Jumamosi, COTU iliwaonya wanachama wake dhidi ya kushiriki maandamano hayo yaliyopangwa, ikibainisha kuwa Jumatatu, Machi 20, 2023, haijatangazwa rasmi kuwa sikukuu ya umma, runinga ya NTV iliripoti.

"Kama shirika mwamvuli la wafanyikazi, tunataka kuwakumbusha wafanyikazi kulinda kazi zao kwa kuripoti kwenye vituo vyao vya kazi," Benson Okwaro, Naibu Katibu Mkuu wa COTU.

"Tunawaomba wafanyakazi wajizuie kushiriki katika shughuli zozote zinazoweza kuhatarisha hali yao ya ajira."

Tamko hilo linafuatia mwito wa wabunge wa Azimio la Umoja One Kenya Coalition Party kwa waajiri kuwaachilia wafanyikazi wao ili wajiunge na shughuli hiyo kubwa.

Hata hivyo, COTU inatoa wito kwa wafanyikazi kutanguliza hali yao ya kuajiriwa na kuacha kushiriki katika shughuli zozote zinazoweza kuhatarisha kazi zao.

Pia muungan ohuo ulisisitiza haja ya vyama pinzani kupata suluhu kwa njia za Amani bila kuitisha maandamano na mihemko ya kisiasa nchini.

"Tunatoa wito kwa pande zote mbili kushiriki katika mazungumzo ya dhati na kutafuta suluhisho la muda mrefu ambalo litakuza maendeleo ya kiuchumi nchini," ilisoma taarifa hiyo kwa sehemu.

COTU pia inaitaka serikali kutanguliza ustawi wa wafanyikazi kwa kukuza ulinzi wa kijamii na kuunda mazingira ya biashara ya amani ambayo yanakuza ukuaji wa uchumi.

Kinara wa upinzani Raila Odinga alitangaza Jumatatu kuwa "likizo ya umma," ingawa ni Waziri wa Mambo ya Ndani pekee ndiye aliye na mamlaka ya kutangaza likizo ya umma, kulingana na sheria.

Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Opiyo Wandayi alitoa wito kwa waajiri kuwaachilia wafanyikazi wao ili kushiriki katika shughuli hiyo kubwa.

Awali, mbunge wa Kapseret Oscar Sudi alitoa onyo kali kwa wafanyikazi wa umma ambao watadaiwa kujiunga katika maandamano hayo wakiacha kazi zao siku ya JUmatatu ya Machi 20.