Washukiwa wawili wa wizi wa kimabavu watoroka kituo cha polisi cha Kakamega

Wawili hao walitoweka kutoka kituo cha polisi cha Kakamega katika hali isiyoeleweka Alhamisi Mei 25.

Muhtasari

• Maafisa wawili wa polisi waliokuwa zamu wakati wawili hao walipotoroka wametiwa mbaroni ili kusaidia katika uchunguzi.

• Kulingana na taarifa ya mkurugenzi wa upelelezi wa makosa ya Jinai kwenye akaunti ya Facebook, wawili hao walitoweka kutoka kituo hicho kwa hali isiyoeleweka Alhamisi Mei 25.

Washukiwa wanaodaiwa kutoweka kutoka kituo cha polisi cha Kakamega.
Washukiwa wanaodaiwa kutoweka kutoka kituo cha polisi cha Kakamega.
Image: FACEBOOK/DCI

Polisi wanawasaka washukiwa wawili wa wizi wa kimabavu waliotoroka kutoka kituo cha polisi cha Kakamega.

Kulingana na taarifa ya mkurugenzi wa upelelezi wa makosa ya Jinai kwenye akaunti ya Facebook, wawili hao walitoweka kutoka kituo hicho katika hali ya kutatanisha siku ya Alhamisi Mei 25.

Denis Indeche,26 alikamatwa siku ya Jumanne na maafisa kutoka taasisi ya utafiti wa uhalifu na Ujasusi baada ya kuwa mafichoni kwa muda.

Indeche, anasakwa kwa kushukiwa kuhusika katika matukio ya wizi wa kutumia silaha Magharibi mwa Kenya, ikiwa ni pamoja na shambulio dhidi ya afisa wa DCI anayeishi Kakamega.

Afisa huyo wa DCI aliponea shambulio hilo la na mareheja mabaya.

Maafisa wawili wa polisi waliokuwa zamu wakati wawili hao walipotoroka wametiwa mbaroni ili kusaidia katika uchunguzi.

Taarifa ya DCI ilitoa wito kwa umma kuwa waangalifu na iwapo watakuwa na taarifa zinazoweza kusaidia kukamatwa kwa washukiwa hao kupiga simu kwa 0800 722 203

Washukiwa hao ni Denis Indeche,26 na Allan Kemoili, 29.