Hata kama nilimpigia Uhuru kura 2017, niliamini Raila alimshinda - Miguna

Wakili huyo alikuwa akielezea sababu za kumuapisha Raila kama rais wa wananchi mnamo Januari 2018.

Muhtasari

• Ulipofanyika uchaguzi naamini kutokana na takwimu zilizokuwepo kuwa Raila alishinda uchaguzi - Miguna.

• Alieleza kwamba hata kama hakuwa anampenda Raila lakini alihisi amedhulumiwa kwa kuibiwa ushindi wake.

Miguna Miguna afunguka kilichosababisha kufurushwa nchini 2018
Miguna Miguna afunguka kilichosababisha kufurushwa nchini 2018
Image: Facebook

Baada ya kuwasili nchini mnamo Octoba 20, wakili Miguna Miguna ameanza kufunguka kuhusu masuala kadhaa ambayo yalisababisha kufurushwa kwake nchini na jinsi uhusiano wake na kinara wa Azimio la Umoja One Kenya Raila Odinga ulivyozorota, licha ya kuwa mwandani wake na hata kumwapisha kama rais wa wananchi.

 Akizungumza katika runinga ya NTV na mwanahabari Joe Ageyo, Miguna alisema kwamba yeye alimpigia Uhuru Kenyatta kura katika uchaguzi wa mwaka 2017 lakini baadae aligundua kuwa Raila alishinda na ndio maana alikuwa mstari wa mbele katika kumwapisha.

Miguna alieleza kuwa kutokana na data alizokuwa nazo, Raila alikuwa ameshinda kura za urais za Agosti 2017. Alisema licha ya kuzozana na waziri mkuu huyo wa zamani na kumchukia, aliamini kuwa angemshinda rais wa wakati huo Uhuru Kenyatta.

“Ulipofanyika uchaguzi naamini kutokana na takwimu zilizokuwepo kuwa Raila alishinda uchaguzi, ingawa sikumuunga mkono, nilikuwa nimekorofishana na Raila Odinga, sikumpenda, kiukweli nilimchukia yangu yote,” alisema Miguna.

Wakili huyo alieleza kuwa licha ya kuidhinisha azma ya Uhuru kuwania urais 2017, alimpinga alipogundua kuwa alidaiwa 'kuiba' ushindi wa Raila. Alisema kwamba kilichomfanya kusimama kidete kupinga matokeo ya Kenyatta licha ya kumpigia kura ni dhana iliyokuwa ndani yake ambayo msingi wake mkuu uliongozwa na utiifu kwa katiba ya Kenya na pia demokrasia.

"Nilisema subiri kidogo, ukweli kwamba niliidhinisha Uhuru na kumpigia kura haimpi kibali cha kuiba uchaguzi wa mtu kwa sababu, kwangu mimi, sheria ni kardinali. Ukuu wa katiba na demokrasia ndio mambo pekee ninayozingatia. Kwa hivyo nikasema kwenye hili, Uhuru umekosea nitakupinga. Mimi nitamuunga mkono mshindi halali ingawa simpendi " Miguna alisema.