Amuua mke wake na kumpigia simu mtoto wao kumtaarifu kabla ya kwenda mafichoni

Uchunguzi wa awali ulibaini kuwa mwili wake ulikuwa na majeraha saba ya kuchomwa kisu tumboni, kifuani na usoni.

Muhtasari

• Mtoto wao ambaye ni mwanafunzi wa chuo kikuu alitaarifiwa na baba yake kuwa ameua mama yake.

• Polisi walianzisha msako dhidi yake ambapo mpaka  Jumatano asubuhi hakuwa amepatikana.

Crime Scene
Image: HISANI

Jumanne, mwanamume mmoja mfanyibiashara katika kaunti ya Nakuru alimuuwa mke wake kwa kumchoma kisu.

Sasa imebainika kwamba baada ya kutekeleza kitendo hicho, mshukiwa Amos Njuguna alimpigia mtoto wake wa kiume simu kumtaarifu kuwa ameua mama yake Winnie Chepkurui kabla ya kuingia mitini.

Katika Makala maalum yaliyochapishwa na jarida la Nation, jirani wao mjini Nakuru aliripoti kwamba baada ya kumuua mke wake, Njuguna alimpigia simu kijana wake mwanafunzi wa chuo kikuu kumtaarifu kuhusu unyama huo.

“Baada ya kumuua mama huyo alimpigia simu mtoto wao kumjulisha juu ya tukio hilo. Alikimbia dakika chache baadaye,” jirani huyo alinukuliwa.

Bw Njuguna alishukiwa kumdunga mkewe kisu mara kadhaa na kuuacha mwili wake kwenye dimbwi la damu. Polisi wameanzisha msako wa kumsaka mshukiwa huyo.

Uchunguzi wa awali ulibaini kuwa mwili wake ulikuwa na majeraha saba ya kuchomwa kisu tumboni, kifuani na usoni.

“Yeye ndiye mtuhumiwa wa kwanza tunayemtafuta ili aweze kutupa taarifa kuhusu kilichojiri. Hata akikimbia tutampata,” akasema Bw Masika, kamanda wa polisi katika kaunti ndogo ya Nakuru Mashariki.

Jirani aliambia polisi kwamba alisikia zogo kutoka kwa nyumba ya wanandoa hao lakini hakufikiria sana, ndipo baadaye akajua kwamba Bi Chepkurui alikuwa ameuawa, Nation waliripoti.