•NPS imesema tabia ya makurutu hao kama ilivyoashiriwa kwenye video inayoenezwa mitandaoni haikubaliki na haiambatani na maadili ya kitengo cha GSU wala polisi kwa ujumla.
•NPS imetoa hakikisho kwamba uchunguzi wa kina kuhusiana na tukio hilo unaendelea na hatua mwafaka zitachukuliwa baada ya ukaguzi wa ndani kukamilika.
Huduma ya polisi nchini (NPS) imelaani vikali tabia na matamshi ya makurutu wa GSU ambao walijirekodi na klipu yao kusambaa kote mitandaoni.
Kupitia kwa taarifa iliyotolewa Alhamisi jioni, NPS imesema tabia ya makurutu hao kama ilivyoashiriwa kwenye video inayoenezwa mitandaoni haikubaliki na haiambatani na maadili ya kitengo cha GSU wala polisi kwa ujumla.
NPS imesema makurutu wote walipitia mafunzo muhimu kuhusiana na kanuni za kidemokrasia za polisi kwa lengo la kuwafanya maafisa wasikivu na wanaowajibika katika kazi yao ya kuhudumia umma. Huduma ya polisi imesema matamshi yaliyotolewa na makurutu hao yanasikititisha sana.
"Tungependa kufafanua na kuwahakikishia umma kwamba tabia iliyoonyeshwa kwenye klipu hiyo haikubaliki na haiakisi maadili ya GSU, Huduma ya Polisi ya Kenya na Huduma ya Kitaifa ya Polisi. Wahitimu wote walipitia mafunzo makali yenye msingi wa thamani yaliyoigwa kwa kanuni za kidemokrasia za polisi na yaliyoundwa ili kuwafanya maafisa wa sheria wasikivu na wanaowajibika katika huduma ya raia.
Kiapo cha utiifu walichokula wakati wa kuhitimu kwao ni kielelezo cha utakatifu wa wajibu wao wa utumishi. Kwa hivyo, matamshi kama yalivyotolewa kwenye klipu yanasikitisha na yamelaaniwa." Taarifa ya polisi ilisoma.
Gsu recruits exited ahead of their pass-out today. Congratulations endeleni mukadumishe usalama sasa. pic.twitter.com/zcOEMF7yvH
— Mike Sonko (@MikeSonko) December 8, 2021
NPS imetoa hakikisho kwamba uchunguzi wa kina kuhusiana na tukio hilo unaendelea na hatua mwafaka zitachukuliwa baada ya ukaguzi wa ndani kukamilika.
"GSU inasifika kwa mafunzo yake mahususi yanayolenga kuzalisha maafisa wenye nidhamu na kuwajibika" NPS ilisema.
Katika video inayoenea mitandaoni, kikundi kidogo cha makurutu wa GSU wenye umri wa ujana kinaoneka kuchangamka wanaposherehekea kukamilisha mafunzo yao.
Maafisa hao wanaonekana wakisakata densi za kisasa kusherehekea kufuzu kwao huku wakijigamba kuhusu ukali wao wanapojiandaa kuanza kuhudumia taifa.
"Ndio hiyo, tiushamaliza.. mabang'a. Tunawakilisha, hii ni red barret.. tunakuja nje. Apana tambua. Hawa ni wale wazii, wabaya. Pa! Pa! Pa!" Maafisa hao wangesikika wakisema.
Wakenya ikiwemo viongozi wameendelea kutoa hisia tofauti kuhusiana na video hiyo baadhi yao wakipendekeza adhabu kwa maafisa husika huku wengine wakiwatetea.