Habari za hivi punde! Rais mstaafu Mwai Kibaki aaga dunia

Muhtasari

• Taifa laomboleza kifo cha rais wa tatu wa Kenya 

Rais mstaafu Mwai KIbaki
Image: state house

Rais wa awamu ya tatu wa Kenya Emilio Mwai Kibaki ameaga dunia.

Kibaki aliaga dunia siku ya Ijumaa akiwa na umri wa miaka 91.

Rais Uhuru Kenyatta alitangaza kifo cha Kibaki katika hotuba yake kwa taifa siku ya Ijumaa.

Kufuatia kifo chake rais Kenyatta ameagiza bendera zote kote nchini kupeperushwa nusu mlingoti kuanzia leo Ijumaa hadi siku ya kuzikwa kwake Kibaki.

Kulingana na taarifa ya rais Kenyatta Kibaki amefariki leo akipokea matibabu.

Kibaki alihudumu kama rais wa tatu wa Kenya kuanzia mwaka 2002 hadi mwaka 2013 alipostaafu na kumuachia usukani rais wa sasa Uhuru Kenyatta.

Kabla ya kuwa rais Kibaki alikuwa amehudumu kama makamu wa rais na waziri katika serikali ya hayati rais Daniel Arap Moi.

Katika hotuba yake rais Kenyatta alimpongeza Kibaki kwa kubadilisha uchumi wa Kenya uliyokuwa umedorora.

Hayati rais Kibaki hajaonekana kwenye umma kwa muda mrefu huku mara ya mwisho ikiwa wakati wa maombolezo ya kifo cha hayati rais Daniel Moi mwezi Februari 2020.

Marehemu kibaki alizaliwa mwaka 1931 katika eneo la Gatuyaini, Nyeri. Alisomea shule ya upili ya Nyeri na kujiunga na shule ya Mangu kwa elimu ya kidato cha tano na sita kabla ya kujiunga na Chuo Kikuu cha Makerere.

Ameacha nyuma watoto Jimmy Kibaki, Wangui Mwai, Tony Kibaki, David Kibaki na Judy Kibaki.