Kenya kugatua vita dhidi ya ufisadi

Serikali imeanzisha mipango ya kupambana na ugaidi katika ngazi za kaunti ili kupunguza tisho la ugaidi kwa nchi.

Rais Uhuru Kenyatta alisema vita dhidi ya ugaidi vimegatuliwa kwa kubuni mikakati ya utekelezaji katika kaunti ili kuzuia na kukabiliana na visa vya misimamo mikali yenye kuzua vurugu.

Mikakati hiyo ya kaunti, iliyobuniwa kuambatana na mahitaji ya kiusalama ya kila moja ya kaunti 47 nchini, inalenga kuwaleta pamoja wahusika katika sekta ya usalama zikiwepo asasi za usalama, watawala, makundi ya kijamii na raia ili kuweka kipaumbele kwa juhudi za pamoja za kukabiliana na ugaidi zinazoweza kupimika na kutekelezwa kwa kipindi fulani.

Uhuru alisema harakati za kupambana na ugaidi zitasaidiwa na utaratibu wa kuhakikisha usalama kwa wanafunzi utakaobuniwa na Wizara ya Elimu. Rais Kenyatta, aliyezungumza alipofungua kongamano la kukabiliana na ugaidi katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa yalioko Gigiri siku ya Alhamisi, alisema Utaratibu wa kuhakikisha Usalama kwa Wanafunzi utaanzishwa katika miezi michache ijayo.

“Lengo lake ni kulinda watoto wetu kutokana na matizo mengi dhidi ya usalama wao ambao unaweza kuwafanya kutumbukia katika mafundisho ya ugaidi”, kasema Rais.

Sherehe za ufunguzi wa kongamano hilo pia zilihutubiwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Gutteres na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika Moussa Faki Mahamat.

Rais Kenyatta alisema mataifa ya Afrika yanahitaji kuwa na mikakati thabiti ya kukabiliana na ugaidi na pia kuweka mipango ya kuwasitisha, kuwarekebisha na kuwarudisha katika jamii wale wanaokana mawazo na mafunzo ya kigaidi.