Mama ajifungua katika seli ya polisi na kuachiliwa kwa dhamana na mahakama

Maafisa wa polisi kutoka Kituo cha Polisi cha Tigoni waligeuka kuwa wakunga wakati mfungwa mmoja alianza kukumbana na maumivu ya kujifungua.

Ann Wanjiru, mkaazi wa Murengeti, Limuru, alisaidiwa na baadhi ya maafisa wa polisi kujifungua mtoto wa kike.

Mama huyo alikuwa anakumbana na mashtaka ya kumpiga mwenzake na alishindwa kujilipia dhamana ya KSh10,000 aliyoamriwa alipe na korti.

Wanjiru alikuwa amezuiliwa katika kituo hicho cha polisi kwa sababu ya hofu ya virusi vya corona ambapo hangeweza kupelekwa katika Gereza la Akina Mama la Lang’ata.

Wakati wa siku ya tukio hilo, afisa aliyekuwa katika zamu alimpata Wanjiru akiwa na maumivu ya kujifungua na kwa upesi afisa huyo alimpeleka katika chumba kisafi.

“Ilikuwa mwendo wa saa moja usiku na tukapatwa bila kujipanga.Wanjiru alijifungua mtoto wa kike mbele yetu," alisema Mwema.

Mwema alikwenda nyumbani kwake na kuchukua blanketi ya kumfunika Wanjiru huku maafisa wengine wakijitokeza na nguo za mtoto.

Kisha mama huyo alipelekwa katika kituo cha matibabu cha Limuru ambapo alifanyiwa uchunguzi pamoja na mtoto wake na kugunduliwa kuwa buheri wa afya.

Walirejeshwa katika stesheni ya polisi ambapo Mwema alikuwa amewatengea chumba chao.

Kisha John Misoi ambaye ndiye anasimamia kituo hicho cha polisi alishauriana na mahakama imuachilie Wanjiru chini ya bondi ya kibinafsi. Misoi na Mwema, ambaye anaongoza idara ya jinsia wamekuwa wakimpeleka Wanjiru kliniki katika Hospitali ya Tigoni Level 4.

Mume wa Wanjiru, George Ndungu alisema wamekuwa wakiomba familia ya mlalamishi kutupilia mbali kesi hiyo.