Mbunge wa Embakasi mashariki Babu Owino kufikishwa mahakani kesho

Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino atafikishwa mahakamani kesho kukabiliwa na mashtaka ya jaribio la mauaji na kutumia vibaya silaha.
Wakati huo huo DJ Evolve anayedaiwa kupigwa risasi na mbunge huyo amefanyiwa upasuaji wa kuondoa risasi iliyokua shingoni mwake.
Mkusanyiko wa habari,
Ajuza wa miaka 86 amepatikana akiwa amebakwa na kuuawa nyumbani kwake huko Embu. Chifu wa Mbeti Kaskazini Jacob Kamongo anasema mwanamke huyo alikua akiishi peke yake na mwili wake ulipatikana na majirani walioanza kumtafuta baada ya kutomwona kwa wiki moja.
Kutoza ushuru mkate, unga wa ngano na mahindi katika juhudi za kukabiliana na upungufu wa bajeti na mikopo ya serikali, sio suluhu na litawaumiza wateja. Mwanauchumi Charles Karisa anasema ingawaje IMF imekua ikisukuma hilo, hii itasababisha mfumko wa bei na haitasuluhisha suala la mikopo.
Polisi huko Mlolongo waliwakamata wanawake watatu wanaodaiwa kuhusika na ulanguzi wa watoto, ijumaa usiku. Naibu kamishna wa eneo hilo Dennis Ongaga anasema wamekua wakiwafuatilia wanawake hao kwa siku kadha. Washukiwa hao watafikishwa mahakamani kesho.
Viongozi wanaomuunga mkono naibu wa rais William Ruto walivurugana na polisi jana walipojaribu kuandaa mkutano katika uwanja wa Nabongo huko Mumias. Patashika lilizuka wakati viongozi hao walipojaribu kuingia kwa nguvu uwanjani humo.
Watu wawili walifariki jana katika ajali kwenye barabara ya Kangundo-Kathiani. Ajali hio ilitokea wakati lori moja lilipogongana ana kwa ana na pikipiki na kuwauwa dereva na abiria wake.