Mbunge wa wajir mashariki Rashid Amin ameshtumiwa kwa kumshambulia mwakilishi wa akina mama wa wajir Fatuma Gedi katika majengo ya bunge mapema alhamisi . kisa hicho kilifanyika katika eneo la kuegesha magari bungeni wakati Bi.Gedi alipokuwa na mwakilishi wa akina mama wa homabay Gladys Wanga walipokuwa wakielekea mkutanoni aliposhambuliwa na Bwana Amin .
Bwana Amin alimshtumu Bi Gedi ambaye ni mwanachama wa kamati ya bajeti kwa kukosa kulitengea eneo bunge lake pesa wakati wa ziara ya hivi karibuni ya kamati hiyo katika kaunti ya Wajir .
Baada ya dakika chache Bw .Amin alimpiga Bi.Gedi ngumi usoni na kumwacha akivuja damu huku Amin akizuiwa na mbunge wa Wajir magharibi Ahmed Kolosh . Bi.Wanga aliyeshuhudia tukio hilo amesema walikuwa pamoja na Gedi wakati alipoviziwa na Bw. Amin . Gedi alikimbizwa katika hospitali ya Karen kwa matibabu na baadaye akahudumiwa na daktari mmoja wa polisi . Suala hilo limeripotiwa katika Kituo cha polisi cha bunge kama OB/20/13/6/2019.