Granit Xhaka aiaga Arsenal baada ya miaka 7

Xhaka alihusika katika jumla ya mechi 297 za Arsenal ambapo alifunga mabao 23.

Muhtasari

• Xhaka alijiunga na klabu ya Ujerumani, Bayer Leverkusen katika mkataba ulioripotiwa kugharimu takriban pauni milioni 21.4.

•Arteta alimsifu kiungo huyo mwenye umri wa miaka 30 wakati akiiaga klabu hiyo na kumtakia heri katika safari yake mpya.

amejiunga na Bayer Leverkusen
Granit Xhaka amejiunga na Bayer Leverkusen
Image: ARSENAL

Klabu ya soka ya Arsenal imetangaza kuondoka na nahodha wake msaidizi Granit Xhaka.

Klabu hiyo yenye maskani yake jijini London ilithibitisha katika taarifa yake siku ya Alhamisi jioni kwamba kiungo huyo mwenye umri wa miaka 30 alijiunga na klabu ya Ujerumani, Bayer Leverkusen katika mkataba ulioripotiwa kugharimu takriban pauni milioni 21.4.

"Granit Xhaka amejiunga na klabu ya Bundesliga ya Bayer Leverkusen kwa uhamisho wa kudumu," klabu ya Arsenal ilitangaza kupitia tovuti yake rasmi.

Nahodha huyo wa timu ya taifa ya Uswisi anaondoka katika klabu hiyo ya Ligi Kuu ya Uingereza baada ya kuichezea kwa takriban miaka saba tangu ajiunge nayo mwezi Mei 2016. Alihusika katika jumla ya mechi 297 ambapo alifunga mabao 23.

Kocha wa Arsenal, Mikel Arteta alimsifu kiungo huyo mwenye umri wa miaka 30 wakati akiiaga klabu hiyo na kumtakia heri katika safari yake mpya.

“Granit amekuwa sehemu kubwa ya klabu yetu kwa muda mrefu. Amejitolea na ubora kwa miaka mingi, akicheza jukumu muhimu katika maendeleo na mafanikio yetu. Anatuacha na heshima na shukrani zetu kubwa. Tunamtakia Granit kila la kheri kwa siku zijazo,” Arteta alisema.

Bayer Leverkusen pia ilithibitisha kumsajili mchezaji huyo wa kimataifa wa Uswizi kupitia mitandao yake rasmi.

"Granit Xhaka amesaini kutoka Arsenal kwa mkataba hadi 2028 kwenye uwanja wa Bay Arena," Leverkusen ilitangaza siku ya Alhamisi jioni.

Katika klabu hiyo ya Ujerumani, Xhaka atavaa jezi namba 34 ambayo alikuwa akiivaa katika Arsenal.