Mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 46 auwawa Kaunti ya Bungoma

Hali ya huzuni imetanda katika kijiji cha Makutano Eneo bunge la Kanduyi Kaunti ya Bungoma baada ya mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 46 kuuwawa na watu wasiojulikana kwa kudaiwa kudungwa dungwa mara kadhaa kwa kisu.

Tom Sifuna Mumewe marehemu anaarifu kuwa alipata habari kuwa wanawe walifika nyumbani kutoka shuleni majira ya jioni na kumpata mama yao kwa jina Irene Sifuna ameuwawa na alipofika nyumbani alimpata mkewe akiwa amelazwa kitandani akiwa uchi na majeraha ya kisu mgongoni huku kisu kilichokuwa na damu pamoja na kamba vikipatikana kando yake.

Hata hivyo maafisa wa polisi wameanzisha uchunguzi kuhusiana na kisa hicho huku wakimsaka mfanyakazi wa boma hilo ambaye anadaiwa kutoweka na kwenda mafichoni baada ya kisa hicho cha kutamausha.