ORODHA: Saratani zinazoongoza kwa kusababisha vifo barani Afrika

saratani
saratani
Barani Afrika saratani zinazoongoza kwa kusababisha vifo ni zile za mlango wa kizazi, saratani ya matiti, ile ya ini, saratani ya tezi dume, Kaposis sarkoma na mitoki.

Saratani ni ugonjwa ambao unaweza kuathiri sehemu yeyote ya mwili na hii hutokana na uharibifu wa seli pamoja na kiini ambacho hubeba vinasaba.

Iwapo kinasaba kitaathirika, seli hukosa mpangilio na mwelekeo na hugawanyika bila kufuata kanuni. Mara nyingine hugawanyika bila kukomaa na bila usawa hali inayosababisha uvimbe kutokana na mrundikano wa seli.

Seli hizi zina uwezo wa kuathiri seli ambazo hazijaathirika na huweza kutoboa hata mishipa ya damu na kusafirishwa kwa mfumo wa damu kutoka sehemu moja ya mwili kwenda sehemu nyingine ya mwili hatua inayofanya uogonjwa huo kusambaa.

Kwa mujibu wa shirika la afya duniani, kumekuwa na ongezeko la saratani katika muongo huu ambapo mwaka 2012, takriban watu 8.2m walikadiriwa kuwa na saratani na walipoteza maisha.

Barani Afrika saratani zinazoongoza kwa kusababisha vifo ni zile za mlango wa kizazi, saratani ya matiti, ile ya ini, saratani ya tezi dume, Kaposis sarkoma na mitoki.

Ongezeko la ugonjwa huo linatokana na mabadiliko ya mfumo wa maisha kama vyakula, kutofanya mazoezi, unywaji wa pombe na uvutaji wa sigara.

Afrika, maambukizi ya kirusi cha HPV na hepatitis B na C yameleta ongezeko la saratani ya mlango wa kizazi na ini. Watu wengi wanaweza kusaidia kwa kutoa elimu na uchunguzi wa afya na kutambua dalili za awali za saratani pamoja na kurekebisha mfumo wa maisha.

Saratani haijapewa kipaumbele kusini mwa jangwa la Sahara kutokana na magonjwa ya kuambukiza kuwa ya kiasi kikubwa.

Tukiangazia eneo la Afrika mashariki hasa Tanzania, ongezeko la wagonjwa wa saratani linaendelea kukuwa kutokana na elimu ambayo inaendelea kutolewa.

Takwimu za Shirika la tafiti za saratani zinaonesha kwamba Tanzania kuna wagonjwa wapya 42,060 kwa mwaka - kati ya hao wagonjwa 28, 610 hufariki kila mwaka ikiwa ni sawa na asilimia 68 ya vifo.

Takwimu za hospitali zinaonesha kuwa wagonjwa wapya 14,028 walihudumiwa mwaka 2018 ikiwa ni sawa na asilimia 33.3 ya wagonjwa wote nchini.

Wagonjwa 7,649 walihudumiwa Ocean road, 2790 Bugando Mwanza, 1050 KCMC, 1322 Muhimbili na 218 Mbeya Rufaa.

Takribani wagonjwa 1000 walitibiwa hospitali katika binafsi. Aidha asilimia 75 ya wagonjwa huwasili wakiwa katika hatua za juu za ugonjwa na vigumu kupona kabisa.

Taasisi ya saratani Ocean road zinaonesha kwamba kumekuwa na ongezeko la wagonjwa wa saratani ukilinganisha na mwaka 2015 ambapo ilipokea wagonjwa 5764 na mwaka 2018 ikapokea wagonjwa 7649.

Kwa jumla visa vipya vya saratani mwaka 2018 vilikuwa 105,5172 huku idadi ya vifo kutokana na ugonjwa huo ikifikia 693,487.

-BBC