Mwanafunzi wa darasa la tano katika shule ya msingi Onyalo huko Migori ameaga dunia baada ya kusakamwa na andazi akijaribu kulimeza ili kulificha kutoka kwa wenzake .Josiah Ombura alikuwa akicheza wakati wa mapumizko ya asubuhi wakati kisa hicho kilipotokea . ‘Marehemu alikuwa akiligawanya andazi moja ili kuwapa wenzake lakini wengi zaidi walipokuja aliamua kulimeza lote lakini likamsakama’ amesema mwalimu mkuu Dedan Odhiambo.
Odhiambo amesema wanafunzi wenzake waliripoti kwamba mwanafunzi huyo hakuweza kuongea na alikuwa akijaribu kupumua .‘Ameripoti shuleni akiwa na furaha na tukio hilo limetutamausha’ amesema mwalimu huyo mkuu .
.
Jaribio la kumfanyia huduma ya kwanza ili kumwokoa na kumpelekea katika hospitali ya rufaa ya Migori limetibuka baada ya kutangazwa kuaga dunia alipofikishwa hospitalini . Chifu wa lokesheni ya Suna ya kati Caleb Ombura ambaye ni mjombake marehemu amesema tukio hilo limewashangaza na polisi wataanzisha uchunguzi baada ya uchunguzi wa mwili kufanyika . Mwili wa mtoto huyo umepelekwa katika hifadhi ya maiti ya Migori .