Silent Killer: Kuwashambulia watu mitandaoni ni jambo hatari

Mashambulizi ya mitandaoni dhidi ya watu mashuhuri na wa kawaida yaani cyber bullying ni tatizo ambalo sasa linafaa kushughulikiwa  vilivyo na mamlaka husika .  Wiki iliyopita,  wakenya wawili nchini walipitia  cheche za mashambulizi kutoka kwa wanamitandao hasa  twitter na kuzua tena mjadala wa iwapo mengi yanafaa kufanywa ili kukabiliana na chuki zinazosambazwa kupitia mitandao ya kijamii .

Caroline Flack

Wa kwanza ambaye hakustahili uvamizi uliolenga maisha yake binafsi ni Brenda Cherotich ambaye serikali ilitangaza kwamba alikuwa amepona virusi vya Corona. Licha ya baadhi ya wanamitandao kutoamini masimulizi yake kuhusu  safari yake nzima ya kuambukizwa ugonjwa huo na baadaye kutengwa katika karantini wakati akipona , wengi walianza kuzisambaza picha zake za  zamani katika jitihada za kumdhalilisha .

Kilichowavunja   wengi nyoyo  ni kuanza kusambazwa kwa picha za utupu za Brenda katika hatua ya kujaribu  kumfanya ajihisi mtu duni .  Baada ya hilo, mtangzaji wa Runinga  Yvonne Okwara alipojaribu kukosoa tabia hiyo naye pia akawekwa chini ya kaa la moto kwa mashambulizi yaliolenga maisha yake bila   kujali  kwamba alikuwa na  haki  ya kutoa maoni yake .

Kinachochochea  umuhimu wa dharura wa kuchukua hatua za kuzuia uenezaji wa  chukio mitandaoni ni kisa cha mapema mwaka huu  ambapo mtangazji wa runinga kutoka Uingereza Caroline Flack alijiua katika hali ya kutatanisha baada ya kuelekezewa chuki chungu nzima katika mitandao ya kijamii . Flack alikuwa mtangazaji wa kipindi cha ‘Love Island’ na kifo chake kiliutukiza ulimwengu na  hasa waliokuwa wakifuatilia vipindi alivyokuwa akishirikishwa. Wengi walishangaa ilikuwaje kwa mtu mashuhuri kama yeye kufika mwisho hadi akaamua kujiua  lakini sasa rafiki zake wa karibu wameanza kutoa ufichuzi wa jinsi Flack alivyosumbuliwa fikra na  mashambulizi kutoka kwa watumiaji wa mitandao .