Tanzania imeagiza wakimbizi kutoka Burundi kurudishwa makwao

Serikali ya Tanzania imeagiza wakimbizi kutoka nchini Burundi kurudishwa makwao, na kusema kua hali ya kiusalama katika taifa hilo sasa imeimarika.

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Tanzania Kangi Lugola ametangaza kuwa wakimbizi 2,000 watarudishwa Burundi kufikia October mosi.

''Azimio la msingi lilikuwa kila wiki wakimbizi lazima wakimbizi elfu mbili wawe wanarejeshwa nchini Burundi lakini tulipokutana na Mamlaka ya Burundi tuligundua kuwa UNHCR ndio wamekuwa wakikwepa jukumu hilo likisema Burundi haina uwezo wakuwapokea wakimbizi 2000 kwa wiki'' Waziri Lugola aliiambia BBC katika mahojiano ya kipeke.

Aliongeza kuwa serikali ya Burundi kupitia waziri wao wa mambo ya nje Pascal Barandagie waliwasilisha ombi lao kwa Tanzania kuelezea kutoridhishwa kwao na utekelezajiwa makubaliano waliofikia hivi karibuni kati ya nchi hizo mbili na shirilka la kuwahudumia wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR.

Bw. Lugola anadai kuwa shirika hilo la wakimbizi lina ajenda ya siri kwasababu linaleta kisingizio ambacho sio cha kweli.

Mbali na maelezo iliyopata kutoka wizara ya Mambo ya nje ya Burundi kwamba nchi hiyo ni salama wazirri Lugola anasema kuwa imeridhisha kuwa wakimbizi hao watakuwa salama wakirudi makwao kwa sababu tangu mwaka 2015 hakuna hata mkimbizi mmoja aliyeingia nchini humo kutoka Burundi kwa kuhofia usalama.

Mashauriano ya wakimbizi wa Burundi kurejeshwa makwao yamekuwa yakiendelea kati ya Mataifa hayo mawili na shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR na Burundi imekuwa ikiiomba Tanzania kuwaachilia wakimbizi wake warudi nyumbani kulijenga taifa lao.

Lakini wakimbizi hao wana usemi wowote kuhusiana na suala hilo?

Waziri wa mambo ya nje wa Tanzania Bw. Kangi Lugola anasema majadiliano hayo hayawahusu wawkimbizi wenyewe moja kwa moja kwa sababu ''hawakuja Tanzania kwa hiari yao''.

''Tukisubiri urudi nchini kwako kwa hiari tutakuwa tunategemea hiari yako wewe binafsi lakini sisi tunaangalia sababu iliyokufanya utoroke nchi yako ilikuwa hoja ya amani na usalama'' alisema.

Anashangaa kwa nini kigezo cha wakimbizi kurudi kwao kwa hiari linakuja na kuongeza kuwa hilo ni hoja ambalo Tanzania linaliangalia kwa ujumla wake badala ya mtu mmoja mmoja. Tanzania inashikilia kuwa sababu iliyoifanya iwapatia hadhi ya ukimbizi raia hao wa Burundi kwa sasa hazipo na kwamba ina kila sababu ya kuwataka warudi makwao.

''Kuna haya makubaliano ya Kimataifa ambayo UNHCR inatumia lakini katika mazingira ambayo sisi tunatumia sheria yetu sasa ni wajibu wa shirika hilo kuwatafutia wakimbizi hao taifa lingine la tatu kama linaona kurudi kwao Burundi kuna matatizo wakati sisi tunasema hakuna matatizo'' Bw. Lugola anasema.