Ushahidi kwamba virusi vya corona vinasambazwa hewani hautabidilisha mbinu za kuvizuia

covid 19
covid 19
Utafiti mpya  unaoonyesha kwamba virusi vya corona  vinasambazwa hewani  hautabadilisha njia za kuuzuia ugonjwa huo,  amesema mtaalam wa afya.

Akizungumza na  gazeti la The Star  siku ya Jumatatu, Profesa Atwoli Lukoye  amesema kutorundikana kwa watu, kutumiwa kwa maski na kunawa mikono kila mara bado ndio njia muhimu sana za kujikinga dhidi ya virusi vya corona.

Hii ni baada ya kundi la  wanasayansi 239  kutoka mataifa 32  kuliandikia barua  shirika la afya duniani  WHO  na kulipa ushahidi huo mpya  wakieleza kwamba matone madogo madogo  ya hewa yanaweza kuwaambukiza watu ugonjwa huo.

Wamesema kuna uwezekano wa maambukizi  hata ndani ya majumba, katika sehemu zenye watu wengi, sehemu zisizokuwa na hewa safi na nyakati mtu havalii maski kwa muda mrefu.

Wanalitaka shirika la WHO kurekebisha mwongozo wake wa jinsi ya kukabiliana na virusi hivyo  baada ya kugunduliwa kwamba matone ya hewa yana uwezo wa kuwezesha  usambaaji wa virusi vya corona.

WHO imekuwa ikishikilia kwamba virusi hivyo husambaa kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine  kupitia matone ya mdomoni au puani  ambayo hutolewa wakati mtu anapokohoa au kupiga chafya au akizungumza

Lakini Atwoli  amesema huenda kuna tofauti adimu sana kati ya matone yalio hewani na matone ya kutoka kwa mtu mmoja hadi kwa mwingine.