Wabunge wa ODM waagizwa kufika mbele ya NCIC

NA NAOM MAINYE

Tume ya uiano NCIC imewaagiza wa wabunge watatu wa ODM kufika mbele yake kuhusiana na matamshi ya uchochezi wanayodaiwa kutoa.

Junet Mohamed ( Suna Mashariki), Babu Owino (Embakasi Mashariki) na mbunge wa zamani Irshard Sumra wanatarajiwa kufika mbele ya tume hiyo Jumatatu wiki ijayo kuandikisha taarifa kuhusiana na madai ya uchochezi kwenye mkutano wa kisiasa katika eneo bunge la Kibra.

Katika mahojiano na gazeti la the star siku Alhamisi, afisa mkuu mtendaji wa tume hiyo Hassan Mohamed alisema kwamba wapelelezi wanaweka pamoja ushahidi kabla ya ripoti kamili kuwasilishwa kwa mkurugenzi wa mashtaka ya umma ili hatua ichukuliwe.

"Upelelezi unaendelea. tumetazama video na wapelelezi wanatafuta ushahidi wa kutosha," alisema Mohamed.
Hata hivyo, Watatu hao wamepuuzilia mbali video hizo.

"Wakati walikuja hapa, walisema kwamba walitaka muda wa kuzitazama video kabla ya kuandikisha taarifa zao. Tulikubali kwamba waje Oktoba 28" alisema.

Mbunge wa Rarieda Otiende Omolo ambaye ndiye wakili wa Junet na Babu Owino alikanusha maadai hayo na kuyataja kama "hila" dhidi ya wateja wake.

"Wapelelezi wametueleza maoni ya upande wao kuhusiana na yaliyosemwa Kibra. Tumeyachukua na tutayaangazia kuona iwapo yataambatana na yetu," Otiende aliwaambia wanahabari.

Afisa mkuu mtendaji wa NCIC Hassan Mohammed alionya wanasiasa hao akisema kwamba hatua itachukiliwa dhidi yao.

"Tume imepokea sauti na video za wanasiasa wakitoa hotuba za uchochezi," alisema

"Video hizo zinachunguzwa upya na tume na mashirika mengine na zikionyesha ukiukaji wa sheria wahusika watachukuliwa hatua." Aliongeza.

Mohamed alibainisha kwamba kampeni katika eneo bunge la Kibra zimekuwa za amani kwa kiwango kikubwa ila amewashtumu wagombea wengine  kwa kutumia lugha ya matusi  na kuchochea wapiga kura. Vile vile, wanaotumia mitandao ya kijamii kukiuka sheria za NCIC hawatasazwa.

"Tume inafuatilia mitandao ya kijamii pia kuhakikisha haitumiki kuchochea vurugu au kueneza matamshi ya chuki au kudhalilisha makabila fulani. Tunawahimiza wananchi kudumisha amani sio tu katika maeneo yanayofanya uchaguzi mdogo ila kwa taifa nzima," alisema.