Waiguru kujua hatima yake siku ya Ijumaa

Spika wa senate  ameatangaza kwamba bunge hilo litafanya kikao siku ya Ijumaa ili kuijadili ripoti ya kamati ya wanachama 11 inayochunguza hoja ya kuondolewa afisini Anne Waiguru kama gavana wa Kirinyaga.

Katika arifa ya gazeti rasmi la serikali iliyochapishwa Juni tarehe 23  maseneta wametakiwa kuwa katika bunge la senate  saa nane unusu mchana siku ya Ijumaa.

Gavana huyo ameshtumiwa na wawakilishi wa kaunti waliomuondoa afisini kwa kutumia vibaya  afisi yake, kukiuka katiba  na kukiuka sheria za uagizaji wa bidhaa.

Pia anashtumiwa kwa kujitengea shilingi milioni 10 kama marupurupu  yake ya usafiri.

Waiguru ameyataja madai hayo kama wongo na njama ya kuhujumu uongozi wake. Akijitetea mbele ya kamati ya wanachama 11 siku ya Jumatano, Waiguru amesema anapigwa vita kwa sababu ya kuunga mkono  mchakato wa BBI.

Endapo   kamati hiyo itapata uhalali wa mojawapo ya madai yanayotolewa na wawakilishi hao huenda wakaidhinisha uamuzi wao wa kumfurusha Waiguru afisini. Uamuzi huo hata hivyo utafanywa kupitia kura ya maseneta.

Endapo  madai hayo yatapuuzwa na  wanachama wengi basi hoja hiyo itashindwa.