Babu Owino kusalia rumande hadi Jumatatu, akanusha mashtaka ya kujaribu kuua

Mbunge wa Embakasi East Babu Owino atasalia rumande hadi Januari 27, Jumatatu wiki ijayo wakati mahakama itakapotoa uamuzi kuhusu ombi la kuachiliwa kwa dhamana.

Babu alistakiwa rasmi siku ya Jumatatu kwa tuhuma za kujaribu kumuua DJ Evolve ndani ya B-Club Ijumaa wiki iliyopita.

Pia ameshtakiwa kwa utovu wa nidhamu akiwa na bunduki. Anasemekana kukosa nidhamu akiwa amebeba bastola na kufyatua risasi moja akimlenga DJ.

Akiwa mbele ya hakimu mkuu Francis Andayi, Babu alikanusha mashtaka yote dhidi yake.

Babu anawalilishwa na mawakili Dunstan Omari, Cliff Ombeta na mawakili wengine watano.

Upande wa mashtaka ulipinga vikali ombi la Babu kuachiliwa kwa dhamana kwamba huenda akavuruga mashahidi kutokana na ushawishi wake katika jamii.

"Anajulikana vyema na mhasiriwa na amejaribu kufanya juhudi kufikia mashahidi hasa babake mhasiriwa," upande wa mashtaka ulidai.

Upande wa mashtaka pia ulidai kwamba mbunge huyo anakabiliwa na mshtaka mengine katika mahakama ya Kibera, madai ambayo wakili wake Cliff Ombeta alikanusha.