Mchekeshaji Akuku Danger afunguka kuhusu afya yake baada ya kulazwa hospitalini mara mbili

Amefichua kwamba chanzo cha kuugua kwake ni ugonjwa wa Sickle Cell Anemia

Muhtasari

•Akuku amewahakikishia mashabiki wake kwamba kwa sasa anajisikia mzuri ziadi na anatumai kurejelea kazi zake hivi karibuni

•Mchekeshaji huyo pia amefichua kwamba chanzo cha kuugua kwake ni ugonjwa wa Sickle Cell Anemia ambao amekuwa akipambana nao tangu utotoni

Akuku azungumzia maendeleo ya afya yake
Akuku azungumzia maendeleo ya afya yake
Image: INSTAGRAM

Mchekesaji wa Churchill Mannerson Ochien'g almaarufu kama Akuku Danger ametoa taarifa kuhusu maendeleo ya afya yake baada ya kuwa anaugua kwa kipindi cha wiki kadhaa.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Akuku Danger amesema kwamba bado anaendelea kupata afueni kadri siku zinavyosonga.

Mchekeshaji huyo ambaye tangu mwishoni mwa mwaka jana amekuwa akipelekwa na kutolewa hospitalini mara kwa mara amewahakikishia mashabiki wake kwamba kwa sasa anajisikia mzuri ziadi na anatumai kurejelea kazi zake hivi karibuni.

"Kwa saa niko sawa. Naendelea kurejesha nguvu kila siku. Naendelea vizuri zaidi. Tutarudi na ubaya" Akuku alisema alipokuwa anashirikisha wafuasi wake katika kipindi cha maswali na majibu kwenye Instagram.

Siku chache zilizopita mchekeshaji huyo aliruhusiwa kwenda nyumbani baada ya kulazwa hospitalini kwa mara ya pili katika kipindi cha mwezi mmoja.

Akuku alilazwa tena hospitalini siku chache tu baada ya kuruhusiwa kutoka baada ya kupatikana na ugonjwa wa moyo, pneumonia na kifua kikuu.

"Tunafurahi kwamba Akuku kwa mara nyingine tena anaruhusiwa kutoka Hospitalini ya Nairobi West. Sasa anaweza kwenda nyumbani na atakuwa anapumzika kitandani kwani bado anatumia dawa. Tunatoa shukrani.  Asanteni sana kwa kusimama na Akuku Danger katika safari hii yote" Mwandani wake Sandra Dacha alitangaza mapema wiki hii baada yake kuruhusiwa kutoka hospitalini.

Akuku Danger hata hivyo anasema kwamba bado hajapata afueni kabisa. Amesema kwamba angali anaendelea kunywa dawa na kupambana kurejesha afya yake kikamilifu.

"Sijapona kabisa lakini tutafika hapo" Amesema.

Mchekeshaji huyo pia amefichua kwamba chanzo cha kuugua kwake ni ugonjwa wa Sickle Cell Anemia ambao amekuwa akipambana nao tangu utotoni