"Fikiria mara mbili, acha kuongea matope, chuki haikusaidii", Huddah amwambia Murugi Munyi

Muhtasari

• Huddah Monroe alimchamba Murugi Munyi kwa kukashfu bidhaa zake za kujipodoa.

• “Biashara yangu ni kama mtoto wangu, kwa hiyo unapoichafulia jina ni sawa sawa na kumtukana mwanangu" - Huddah

Huddah Monroe na Murugi Munyi
Image: Instagram

Mwanasosholaiti Huddah Monroe amejitosa katika uwanja wa vita vya maneno baina yake na mkuza maudhui wa mtandao wa YouTube Yummy Mummy almaarufu Murugi Munyi.

Ugomvi huu wa kutupiana cheche kali za maneno ulianza pindi Murugi Munyi aliposema kwamba bidhaa za kujipodoa zinazouzwa na kampuni ya mwanasosholaiti Huddah Monroe zilikuwa zimewekwa katika vifurushi visivyofutia ambapo ilimchukua zaidi ya mwezi mmoja kuvifungua huku vikimletea kumbukumbu za kadi wanazotomiwa watu kuwatakia kheri njema ya mafanikio – success cards.

Murugi Munyi pia alizidi kurusha vijembe zaidi kwa bidhaa hizo za kujipodoa huku akisema kwamba bidhaa zote ziko na maagizo ya matumizi yanayofanana licha ya bidhaa hizo kuwa tofauti kama hasi na chanya.

Maneno haya yalikuwa kama kisu chenye makali kuwili kilichokuta mfupa wa Huddah ambapo alichemka vikali kama mvinyo wa kiasili uliokolezwa chachu na kuamua kumjibu Murugi Munyi kwa kashfa kali huku akifikia mpaka hatua ya kumtupia maneno kuhusiana na upasuaji alioufanyia mwili wake kupunguza ufuta, kwa lugha ya kimombo, Liposuction.

Huddah aliandika kwa machungu katika mfululizo kwenye instastories zake huku akisema kwamba biashara yake ndio kama mboni la jicho lake na kuikashifu ni kama kukitumbukiza kitumbua chake mchangani.

“Biashara yangu ni kama mtoto wangu, kwa hiyo unapoichafulia jina ni sawa sawa na kumtukana mwanangu. Hujui ni kwa muda upi na ni jitihada kiasi gani tumeweka mpaka kuifikisha biashara hii hapa ilipo sasa na bado unaketi tu kwenye nyumba yako ya kizamani ukizungumza pumba. Fikiria mara mbili, wenye chuki huwa hawafaulu,” aliandika Huddah.

Matamshi haya ya kashfa kutoka kwa Murugi Munyi kuhusu bidhaa za kujipodoa za kampuni ya Huddah yalionekana kuwaguza wengi ambao walijitokeza kumtetea Huddah na kusema kwamba huenda Murugi Munyi ni mwenye nongwa tu ya kuchukia mafanikio ya mwanamke mwenziwe.

“Yummy Mummy ni mwenye chuki tu. Nafikiri anasumbuliwa na tatizo la kutojithamini kwa kweli kwa sababu wewe si mtu wa kwanza anakashfu bidhaa zako,” shabiki mmoja alimwandikia Huddah.

Huddah alizidisha ugomvi huo kwa kusema kwamba kila mtu anamchukia Murugi Munyi na ndio maana upasuaji wake wa liposuction ulienda kinyume na matarajio yake na kusema kwamba amekuwa akitafuta kitu cha kumpa kiki mtandaoni na hatimaye kuipata kwa kukashfu bidhaa zake.