•Siku ya kuzaliwa ya Lulu inakuja siku sita baada ya siku ya kuzaliwa ya Rashid Abdalla.Lulu Hassan pia alimsifu mume wake siku yake ya kuzaliwa.
Mtangazaji maarufu Rashid Abdalla amemsifu mke wake Lulu Hassan kwa maneno matamu ya mapenzi mnamo siku yake ya kuzaliwa.
Rashid katika chapisho la Instagram alimfananisha Lulu Hassan na tamthilia endelevu inayogusa maisha ya wengi huku akiongezea kuwa mke huyo wake ndiye mtu pekee anayefahamu uzuri wa ubaya wake na kutathmini ubaya wa uzuri wake.
"Aliyekupa jina Lulu alijua fika kuwa utayapa thamani maisha ya wengi kwa kile kidogo Mungu anchokujalia. Wewe ndiye mtu pekee unayejua uzuri wa ubaya wangu na kutathmini ubaya wa uzuri wangu, Happy Birthday Mrs Mwajita, " alisema Abdalla.
"Nimefikiria sana kile cha kuandika lakini mwishowe nimeishia kujiuliza kipi cha kuandika. Nimetaka sana nisikose cha kuandika lakini mwishowe nikaogopa kukosea cha kuandika," aliongezea Rashid.
"Kheri ya siku ya kuzaliwa Boss lady, mwanamke mwenye roho ya dhahabu," alisema Saada Fateh, mwigizaji wa kipindi cha Sultana.
Rashid Abdalla na Lulu Hassan mbali na kuwa ni wanandoa pia ni watangazaji wenza katika programu ya Nipashe kwenye runinga ya Citizen tangu mwaka wa 2018. Hilo lilijiri baada ya Kanze Dena kuondoka Citizen baada ya kupata kazi katika Ikulu awamu ya aliyekuwa rais Uhuru Kenyatta.
Rashid na Lulu wana watoto watatu. Pamoja, wanamiliki studio maarufu ya uigizaji ya Jiffy Pictures ambayo imetengeneza vipindi kama vile Maza, Maria, Huba, Moyo ,Sultana kati ya nyinginezo.
Rashid Abdalla kabla ya kufanya kazi kwenye runinga ya Citizen alikuwa katika kituo cha QTV kabla ya kufungwa kisha baadaye akafanya kazi katika kituo cha NTV.