Chimano wa Sauti Sol azungumzia suala la kupata mtoto

Muhtasari

•Chimano ambaye takriban miezi mitatu iliyopita  alikiri kuwa shoga amesema kwamba kupata mtoto ni jukumu kubwa ambalo bado hayuko tayari kulichukua.

•Mwanamuziki huyo hata hivyo hajatupilia mbali uwezekano wa kupata mtoto katika siku za usoni.

Image: INSTAGRAM// CHIMANO

Mwanamuziki wa bendi ya Sauti Sol, Willis Austin Chimano ameweka wazi kwamba kwa sasa hayupo tayari kupata mtoto. 

Chimano ambaye takriban miezi mitatu iliyopita  alikiri kuwa shoga amesema kwamba kupata mtoto ni jukumu kubwa ambalo bado hayuko tayari kulichukua.

"Kwa sasa bado nakua. Kupata na watoto sio kama alama ya heshima ambayo nahitaji kupata. Kupata watoto ni jukumu. Ni suala kubwa," Chimano alisema akiwa kwenye mahojiano na Mpasho.

Mwanamuziki huyo hata hivyo hajatupilia mbali uwezekano wa kupata mtoto katika siku za usoni.

"Nitaona kama nitapata watoto. Nikiwa katika hali inayoniruhusu. Kwa sasa hapana," Alisema.

Mwishoni mwa mwaka jana mwanamuziki huyo alithibitisha madai ambayo yamekuwepo kwa miaka kuwa yeye ni shoga.

Chimano aliwahimiza Wakenya kukubali dunia ya sasa imebadilika na kuheshimu imani za watu wengine.

"Friday Feeling ni wimbo ambao unawakilisha tamaduni za jamii ya LGBTQ, ni kielelezo cha tamaduni za jamii ya mashoga, ambayo mimi ni mmoja wao, kwa hivyo hizo ni hisia zangu za kwanza za mimi ni nani, naweka kila kitu wazi kuanzia sasa hakuna kujificha jificha tena, ni 2021," Chimano alisema.