"Wakati ukifika, umefika!" Video ya kihisia ya Mr Ibu katika siku zake za mwisho yaibuka (+video)

Alizungumza kuhusu kukutana na mwimbaji huyo mbinguni baada ya maisha ya duniani na kula pamoja na malaika.

Muhtasari

• Video ya Mr Ibu akimzungumzia kwa upendo mwimbaji Rude Boy kabla ya kifo chake imeibuka kwenye mitandao ya kijamii.

•Mr Ibu alifariki kutokana na mshtuko wa moyo mnamo Machi 2, 2024.

Bw John Okafor hospitalini.
Image: HISANI

Kanda ya video ya marehemu muigizaji wa Nigeria John Okafor almaarufu Mr Ibu akimzungumzia kwa upendo mwimbaji Rude Boy kabla ya kifo chake imeibuka kwenye mitandao ya kijamii.

Katika video hiyo iliyoshirikishwa na msanii wa bendi ya P-Square Rude Boy kwenye mtandao wa Instagram, marehemu muigizaji huyo alisikika akimsifia Rude Boy na kumshukuru kwa sapoti yake.

Alizungumza kuhusu kukutana na mwimbaji huyo mbinguni baada ya maisha ya duniani na kula pamoja na malaika.

“Rudeboy! Ooh Mungu wangu! Sijui nianzie wapi lugha yangu. Lakini kila kitu kinatokea kwa wakati wa Mungu mwenyewe. Wakati ukifika, umefika,” Mr Ibu alizungumza na mwimbaji Rude Boy kutoka kwa kitanda chake hospitalini.

Aliongeza, "Rudeboy, ikiwa hutafika mbinguni, niite nama [nyama]. Utakwenda mbinguni na sisi tutaketi mbele ya malaika na kula pamoja. Maisha yako hayabaki vile vile.. Watu watakuwa wakizungumzia leo ni, ‘Imekuwaje? Lakini Ibu na P-Square, wao si wazazi sawa.’ Lakini nawaambia, wazazi hawaji.”

Katika video hiyo iliyorekodiwa hospitalini, mtumbuizaji huyo aliyeaga na umri wa miaka 62 alionekana dhaifu alipokuwa amelala kwenye kitanda cha mgonjwa. Alikuwa na mirija ya dawa iliyounganishwa na mwili wake.

Mr Ibu alifariki kutokana na mshtuko wa moyo mnamo Machi 2, 2024.

Mchekeshaji huyo alikata roho katika Hospitali ya Evercare nchini Nigeria siku ya Jumamosi, akiripotiwa kufariki dunia akiwa katika hali ya kukosa fahamu.

Matatizo ya afya ya Bw Ibu yalijulikana kwa umma Oktoba mwaka jana wakati familia yake iliposambaza video kwenye mitandao ya kijamii ikimuonyesha nyota huyo wa Nollywood akisherehekea siku ya kuzaliwa kutoka kwa kitanda chake hospitalini.

Katika video hiyo, aliwaomba mashabiki wake usaidizi wa bili za matibabu, na kusababisha uungwaji mkono mkubwa.

Katika ombi lake, alisema, "Wapendwa watu wema wa Nigeria, tunategemea msaada wenu wakati huu tunapouhitaji zaidi... Ninapozungumza na wewe, bado nimelazwa hospitalini; mkurugenzi wa matibabu wa hospitali hii alisema kuwa suluhu bora zaidi ni, ikiwa wazo lake jipya halitafanya kazi, wazo bora ni kukata mguu wangu."

Bw Okafor alijizolea umaarufu miongo miwili iliyopita na vichekesho vya Nigeria "Mr Ibu," ambavyo baadaye vilikuja kuwa utambulisho wake.

Filamu hii bado inachukuliwa kuwa mojawapo ya shoo bora zaidi ya vichekesho katika tasnia ya filamu ya Nigeria.

Katika kazi yake yote iliyochukua zaidi ya miongo miwili, aliendelea kushiriki katika filamu nyingine nyingi mashuhuri za Nollywood.