(+video) Museveni amtaka mwanawe Muhoozi kuondoka Twitter mara moja

Amri hii ya rai s inakuja wiki chache tu baada ya mwanawe kutoa matamshi ya uchochezi kuhusu kuliteka jiji la Nairobi.

Muhtasari

• Hata hivyo, Museveni alisisitiza kwamba Twitter haina ubaya bali tatizo lipo pale kwa kile mtu anatweet.

Rais wa Uganda Yoweri Museveni ameweka wazi kwamba atamshrutisha jenerali mkuu wa majeshi ya Uganda, Muhoozi Kainerugaba ambaye pia ni mwanawe kukoma kutumia mtandao wa Twitter.

Museveni ambaye alikuwa na mahojiano ya kipekee na mwanahabari wa Kenya Sophia Wanuna alisema kwamba mtandao wa Twitter si mbaya bali kinachozingatiwa ni kile ambacho mtu anapakia kule.

“Unatazamia kumwambia Muhoozi kutoka Twitter pengine?” Wanuna alimuuliza Museveni.

“Jenerali Muhoozi ataondoka Twitter. Tumekuwa na mjadala huu, unajua Twitter sasa hivi ni njia ya kisasa ya kuwasiliana, na yeye ameungana na vijana wenzake ambao anafanya mambo nao, lakini suala ni kuhusu ni kile unachotweet,” Museveni alijibu.

Shinikizo la kumtaka Muhoozi kukoma kutumia mtandao wa Twitter linakuja wiki mbili baada ya tweets zake kuwaghadhabisha Wakenya ambapo alisema kwamba ingemchukua muda wa wiki mbili tu kuliteka jiji la Nairobi.

Katika msururu wa tweet hizo ambazo ziliibua vita vya maneno baina ya Waganda na Wakenya, Muhoozi aliwasha moto huo kwa kusema kwamba yeye na majeshi yake ya Uganda wangechukua muda huo mchache zaidi kuweka Nairobi chini ya himaya yao na yeye angechagua kuishi mtaa mmoja kati ya mitaa ya kifahari ya Westlands au Riverside.

Baada ya kushambuliwa vikali na Wakenya, Jenerali huyo alipoa na kuonekana kujutia maneno yake dhidi ya Wakenya. Baadae babake, rais Yoweri Museveni aliandika kwenye Twitter akiwaomba Wakenya msamaha kutokana na chukizo la matamshi na mwanawe.