Mwanablogu wa masuala ya chakula Holy Dave afikishwa mahakamani kwa kosa la kumpiga mwanamume Kilimani

Mwathiriwa alijeruhiwa sana upande wa kushoto wa uso karibu na jicho na nguo zake zilikuwa zimelowa damu.

Muhtasari
  • Holy Dave, ambaye jina lake halisi ni David Kimanthi, alishtakiwa mwezi Oktoba na alikuwa mahakamani kwa kutajwa kwa kesi yake ya shambulio
Mwanablogu wa masuala ya chakula Holy Dave
Image: ANNETTE WAMBULWA

Mwanablogu maarufu wa vyakula na Msanii wa Injili Holy Dave alifikishwa mbele ya mahakama ya Kibera kwa madai ya kumpiga mfanyabiashara katika klabu moja Oktoba 2022.

Holy Dave, ambaye jina lake halisi ni David Kimanthi, alishtakiwa mwezi Oktoba na alikuwa mahakamani kwa kutajwa kwa kesi yake ya shambulio.

Alikuwa amekana mashtaka ya shambulio hilo.

Ilidaiwa kuwa Oktoba 1, mwaka jana katika klabu ya Kilimani, kinyume cha sheria alimvamia Keem David na kumdhuru mwilini.

Kulingana na rekodi za polisi, msanii huyo ambaye yuko nje kwa dhamana anadaiwa kumpiga Keem na chupa ya pombe wakati wa ugomvi katika kilabu hicho.

Mashahidi wanasema kwamba Keem alikuwa ameketi katika sehemu ya VIP na marafiki wawili na wakati rafiki mwingine kutoka meza tofauti aliamua kujiunga nao.

Rafiki huyo alisema alizuiwa na mlinzi kujiunga na meza ya Keem na akaenda kuingilia kati kwa niaba yake ndipo Holy Dave alipoibuka.

Inadaiwa kuwa alitaka kujua kwa nini Keem alikuwa akimtetea rafiki yake kutoka kwa mwana usalama na katika makabiliano hayo, inadaiwa alimpiga upande wa kushoto wa uso wake.

Mwathiriwa alijeruhiwa sana upande wa kushoto wa uso karibu na jicho na nguo zake zilikuwa zimelowa damu.

Holy Dave na Keem walisindikizwa na walinzi nje ya klabu. Kesi hiyo iliripotiwa kwa polisi na Holy Dave alikamatwa na kushtakiwa kwa kosa la kushambulia.

Polisi pia wamepata picha za CCTV za tukio hilo ambazo zitatumika kama ushahidi katika kesi hiyo.

Holy Dave pia alikuwa ameripoti kwa polisi kwamba alipata jeraha usiku huo kwenye kidole chake cha kulia.