MP Babu Owino akosoa nyongeza ya mishahara kwa wabunge na maafisa wengine wa serikali

Licha ya kuwa mmoja wa wabunge watakaonufaika na nyongeza hiyo, Owino amekosoa vikali hatua hiyo akisema kwamba imekuja wakati mbaya ambapo Wakenya wengi wanahangaika kimaisha.

Muhtasari

• "Inasikitisha kuongeza mshahara ilhali Wakenya hawana kazi, Wakenya hawana mitaji ya kuanzisha biashara, Wakenya hawana pesa za kulipia karo za shule, Hakuna pesa za dawa." alisema.

BABU OWINO
BABU OWINO

Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino amekosoa vikali nyongeza ya mishahara kwa wabunge na maafisa wengine serikalini.

Hii ni baada ya tume ya mishahara, SRC kubainisha kwamba viwango vya mishahara ya wabunge na maafisa wengine serikalini vitaongezwa kuanzia Julai mosi, ambayo ni siku mbili zilizopita, kumaanisha kwamba tayari viwango hivyo vpya vimeshatekelezwa katika mishahara ua mwezi huu wa Julai.

Hata hivyo, licha ya kuwa mmoja wa wabunge watakaonufaika na nyongeza hiyo, Owino amekosoa vikali hatua hiyo akisema kwamba imekuja wakati mbaya ambapo Wakenya wengi wanahangaika kimaisha.

“Wabunge na maafisa wengine wa serikali hawafai kuongezwa hata sarafu moja. Inasikitisha kuongeza mshahara ilhali Wakenya hawana kazi, Wakenya hawana mitaji ya kuanzisha biashara, Wakenya hawana pesa za kulipia karo za shule, Hakuna pesa za dawa. Sema HAPANA kwa nyongeza ya mshahara,” Babu Owino alisema kupitia kurasa zake mitandaoni.

Kwa mujibu wa SRC, Wabunge na maseneta, ambao mshahara wa sasa ni Sh725,502, malipo yao yataongezwa hadi Sh739,600 kila mwezi.

Malipo ya magavana yamerekebishwa kutoka Sh957,000 hadi Sh990,000 huku yale ya Mbunge wa Kaunti (MCA) yakiongezeka kutoka Sh154,481 hadi Sh164,588 kila mwezi.